Saturday, October 13, 2012

Waislamu waonyesha makucha yao kwa mara nyingine tena • Wachoma, wavunja makanisa, wapora vifaa vya ibada

KUNDI kubwa la Waislamu wenye imani kali, jana lilizusha vurugu kubwa zilizoambatana na kuchomwa moto na kuharibiwa kwa makanisa manne ya Kikristo jijini Dar es Salaam, katika kile kilichoelezwa kuchukizwa na kitendo cha kijana mmoja wa Kikristo aliyedaiwa kukimwagia haja ndogo kitabu kitakatifu cha Kurani.
Waislamu hao waliokuwa na jazba kubwa, walichukua hatua ya kufanya uharibifu huo, baada ya kushindwa kwa jaribio la kukiteka kituo kidogo cha polisi cha Mbagala wilayani Temeke kwa nia ya kumchukua kijana anayetuhumiwa kufanya tukio hilo, Emmanuel Josephat (14) ili wamuue kwa kumchinja hadharani kama adhabu kwa kosa hilo.
Vikosi vya polisi wenye silaha na mabomu ya machozi na maji ya kuwasha walipambana na Waislamu hao ambao walizidi kuongeza kila dakika, hivyo kufunga shughuli zote za kijamii katika barabara ya Kilwa, eneo lote la Mbagala.
Wakiwa na silaha za mawe, kundi hilo lilivamia mitaani na kuchoma Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Mbagala Zakhem, na lile la Assembly of God (TAG), huku wengine wakiharibu Kanisa la Anglican, kuvunja vioo katika kanisa la Wasabato, na kuchukua vifaa vya muziki na ibada na kuviunguza hadharani.
Waislamu hao waliyaponda mawe na kuyaharibu magari ya polisi namba T 142 AVV, PT 0966 na T 325 BQP, basi la Kampuni ya Usafirishaji Dar es Salaam (UDA) na gari la waandishi wa habari kutoka Clouds.
Jitihada za Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Polisi wa Temeke, David Misime, kujaribu kuzuia kuenea kwa ghasia hizo kwa kuwatumia viongozi wa Kiislamu, zilionekana kugonga mwamba kutokana na viongozi hao kuwatetea waumini wao.
Viongozi wa dini hiyo wakiwemo Sheikh wa Wilaya ya Temeke, Mohamed Kingo, Katibu wa Vijana Bakwata, Abdulkarim Michael Fulano na Sheikh wa Taasisi na Jumuiya za Waislamu, Faridi Salehe Ahmed kukaa kikao na Kamanda Misime, walifikia muafaka wa kuwatuliza Waislamu hao, lakini hali iliendelea kuwa mbaya.
Chanzo cha vurugu hizo ni ubishani wa kitoto uliozuka baina ya mtoto Emmanuel na mwenzake Zakaria Hamis (12) anayesoma Shule ya Msingi Chamazi, Jumatano wiki hii.
Inadaiwa kwamba, Zakaria alimwambia Emmanuel ambaye pia ni jirani yake, kwamba msahafu huo ni mtakatifu na kwamba mtu yeyote ambaye angeuharibu kwa jambo lolote, iwe ni kuuchana kwa makusudi, kuutemea mate ama kuukojolea angekufa pale pale, au kugeuka mjusi.
Katika ubishi huo, Emmanuel aliamua kukojolea msahafu huo, akitaka kuona kama kweli angekufa ama kudhurika, jambo ambalo halikumpendeza rafiki yake ambaye alikwenda kuwaeleza wazazi wake.
Baba mzazi wa Zakaria, aliwaambia waandishi wa habari kwamba, kutokana na tukio hilo alilazimika kwenda kwa wazazi wa Emmanuel na kisha kwenda kwa mjumbe ambaye aliwaelekeza kwenda kituo cha polisi kuandikisha maelezo.
Wazazi wote walikubaliana kuyamaliza mambo hayo, kwa kumwonya mtoto huyo, lakini habari za kuaminika zinasema kuwa baadhi ya viongozi wa Kiislamu hasa msikiti wa Chamazi, waling’aka na kutaka jambo hilo lifikishwe ngazi za juu za uongozi wa Kiislamu.
Viongozi wa Kikristo
Katika hatua nyingine, viongozi wa Kikristo walikataa kuzungumza jambo lolote kutokana na vurugu hizo na kuchomwa kwa makanisa yao.
Jitihada za kuwapata askofu wa KKKT, Anglikani, TAG na Sabato hazikuweza kuwafanya wazungumze lolote, kila mmoja kudai kwamba jambo hilo ni zito na lingetolewa maamuzi kamili leo.
Hadi tunakwenda mitamboni zaidi ya Waislamu 100 walikuwa wamekamatwa, huku vurugu ziliendelea kupinga kukamatwa kwa wenzao na Jeshi la Polisi, licha ya kuombwa na viongozi wao kuwa watulivu na warejee nyumbani kwa kuwa jambo hilo sasa linashughulikiwa na mamlaka za juu.
Kwa muda sasa kumekuwa na matukio ya kuandamana na wakati mwingine kuharibu mali katika matukio kadhaa ya kupinga kile kinachoonekana kuwa dhulma kwa Waislamu.
Hivi karibuni, kundi kubwa la Waislamu waliandamana kwenda Wizara ya Mambo ya Ndani kushinikiza wenzao waliokamatwa kutokana na suala la sensa kuachiwa.
Kadhalika, Waislamu hao waliandamana kutaka kuondolewa madarakani kwa Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa, Dk. Joyce Ndalichako na hivi karibuni wakaandamana kulaani filamu inayodaiwa kumdhalilisha Mtume Mohammad (SAW) iliyotengenezwa na raia mmoja wa Marekani.

No comments:

Post a Comment