Tuesday, October 23, 2012

Kwa hotuba ya J.K kwa vijana wa uvccm ni kweli Kikwete ni Chaguo la Mungu. Katumwa na Mungu kuiua CCM kwa maslahi ya taifa.

NIMESHINDWA kuamini kama habari zilizovuma kwenye vyombo vya habari jana zikimkariri Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jakaya Kikwete, akilalamikia mambo kadhaa ndani ya chama chake kama zimetoka kinywani mwake.
Na labda nichukue fursa hii kuwatahadharisha tena wanasiasa wa ndani ya CCM na watendaji wa serikali yake, wanaofanya kazi karibu sana na rais huyu. Wengi wamejikuta majeruhi wa siasa zake kwa kuwa anachokisema mdomoni sicho kilichoko moyoni.
Samwel John Sitta atakuwa shahidi wangu wa kwanza maana nilitumia makala nzima kumwonya na kumtahadharisha juu ya kitendo cha JK kwenda mpaka Urambo kuzindua ofisi ya mbunge wa Urambo na kumwaminisha kwamba yuko pamoja naye katika harakati zake za kugombea tena ubunge na hatimaye uspika.
Nilimwambia kwamba asiyumbe akaacha kusimamia utekelezaji wa serikali kwa maazimio ya Bunge kuhusu kashfa ya Richmond. Alinisikia, lakini hakunielewa, muulize alivyokujakulia baadaye akidai eti sifa zote za kuwa spika alikuwa nazo isipokuwa moja tu: “awe ni mwanamke.”
Na hii moja haijatamkwa kwenye katiba wala kwenye sheria yoyote ya nchi wala kwenye kanuni za Bunge, wala kwenye kanuni zozote, bali maazimio ya kikao kilichoongozwa na JK, na pengine maazimio yake kupitia kwenye kikao.
Jana kaibuka na kali zaidi. Gazeti dada la hili, jana lilisema: Makundi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), yanaonekana kumwelemea Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, na sasa ameamua kutumia mkutano mkuu wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT), kukemea vitendo vya kudhalilishana na makundi wakati na baada ya uchaguzi.
Rais Kikwete pia alionya juu ya vitendo vya rushwa vinavyozidi kushamiri ndani ya chama hicho akisema kuwa visipochukuliwa hatua mapema, kuna hatari ya kukifikisha chama katika hatua mbaya.
Gazeti lilisema akifunga mkutano huo wa nane wa uchaguzi UWT, Rais aliwataka kufanya jitihada za kupunguza mgawanyiko uliotokea baada ya uchaguzi wao uliomalizika hivi karibuni.
Alisema imekuwa ni hulka sasa hasa baada ya kumalizika uchaguzi kwa wanachama kuendeleza na kuwekeana uhasama kama uliokuwepo wakati wa kampeni.
“Itakuwa ni aibu sana na ajabu, pia utakuwa hujatenda haki kwa kumbagua ambaye hakukuchagua; natolea mfano kwangu katika uchaguzi uliopita, Prof. Mark Mwandosya hakushinda, lakini kwenye serikali yangu nilimuweka licha ya kuwa nilifanyiwa mambo ya ajabu sana ambayo ni vigumu kuyavumilia, lakini kwa mwanasiasa, lazima uwe mkomavu.
“Kweli tusipokemea vitendo hivi na kuviacha vikiendelea, tutakipeleka chama mahali pabaya, ninasikitika sana kusikia hata wanawake sasa wanajihusisha na utoaji rushwa ili kununua nafasi za uongozi kitu ambacho ni hatari sana,” alisema Kikwete.
Alifafanua kuwa chama kinakoelekea si kuzuri ni lazima zifanyike jitihada za mabadiliko.
Mahali kwingine nimesema kwamba hakuna rais aliyepata bahati ya uongozi wa taifa hili wakati wa vyombo vingi vya habari, kama Kikwete.
Ni kweli kwamba uhuru kamili wa vyombo hivi vya habari bado ni ndoto, lakini umeongezeka kwa nguvu kutokana na kuongezeka kwa vyombo vyenyewe. Ni kwa sababu hiyo vimejitokeza vyombo kadhaa kama gazeti hili ambavyo vinaiweka nchi mbele daima na kusimamia ukweli na hivyo kuweza kusema ukweli bila kuogopa.
Kikwete ni rais ambaye amevunja rekodi ya kuelezwa ukweli, kuaswa, kukosolewa, kupewa maoni, kukanywa na hata kuelekezwa mambo mengi katika utawala wake kiasi kwamba angesoma na kufuata hata nusu tu ya yale anayoandikiwa kwenye vyombo vya habari, angekuwa rais bora kuliko wote ikizingatiwa nguvu kubwa ya sapoti ya Watanzania iliyomwingiza madarakani kwa mara ya kwanza kwa asilimia 80.2.
Katika utawala wake, hakuna kitu kimepigiwa kelele na JK kushauriwa mara nyingi kama suala la mtandao uliomwingiza madarakani. Katika marais wote wanne walioongoza taifa hili, hakuna rais aliwahi kuutafuta urais kwa udi na uvumba kama Rais Kikwete. Mwalimu Nyerere alipambana kutafuta uhuru na uhuru ulipopatikana akajikuta anachaguliwa yeye kuwa Waziri Mkuu. Baadaye baada ya nchi kuwa jamhuri kamili pia wenzake walimwona wakamwambia unafaa kuwa rais wetu.
Alipong’atuka Mwalimu na zamu ikawa ni ya Zanzibar, wazee wa Zanzibar walimpendekeza Ally Hassan Mwinyi na akapigiwa kura kuwa rais wa Jamhuri. Baada yake hakuna aliyetegemea kwamba Benjamin Mkapa angekuwa rais. Watani wake walipenda sana kumtania kwamba Kenneth Mkapa, mchezaji beki namba tatu wa timu ya Yanga wakati huo alikuwa ni maarufu kuliko Benjamin Mkapa. Lakini wenzake walimwona ikiwa ni pamoja na Mwalimu.
Wakamshawishi kuchukua fomu, wakampigia debe na hatimaye akawa rais wetu baada ya kumshinda Kikwete ambaye aliingia kwenye kinyang’anyiro si kwa kuombwa na watu, bali kwa kuutamani yeye urais akakaa chumbani yeye na mwenzake Lowassa na wakakubaliana kwamba wachukue fomu halafu atakayekuwa rais amteue mwenzake kuwa waziri mkuu.
Baada ya kushindwa na Mkapa, ndipo alipofanya kitu cha ajabu ambacho hakikuwahi kufanyika hapa nchini na sasa nashangazwa na pale anapojidai anasikitishwa nacho. Wakati Mkapa akihangaika huku na kule kujenga uchumi wa nchi kwa miaka kumi ya uongozi wake, Kikwete alikuwa busy kuunda kundi la mtandao ambalo naamini kabisa lilifikia mahali pa kumtengenezea umaarufu ambao hata hakuwa nao ili tu aje kushinda urais 2005.
Ninaamini ndani ya dhamiri yangu kwamba kundi la mtandao lilitumia kila aina ya njia, halali na haramu, katika kufanikisha mpango wake wa kumwingiza Kikwete Ikulu. Moja ya njia ni kugawa wanachama na viongozi wa chama chake katika makundi kama alivyosema kwamba kundi la Mwandosya lilipambana naye. Ya pili ilikuwa ni kutumia rushwa kama ambavyo ameshindwa kukanusha habari za viongozi wa vyama vya upinzani kwamba pesa za EPA zilizoporwa Benki Kuu zilitumika kumwingiza madarakani.
Mkakati mwingine haramu ulikuwa ni kutumia vyombo vya habari kuandika habari za hovyo juu ya wagombea wenzake, hata kama hazina ukweli kama ambavyo waziri mkuu wa wakati huo, Sumaye, alipofikia mahali akasema “mtu anayetumia kalamu kuwadhibiti wapinzani wake, akishachukua madaraka atatumia risasi kuwadhibiti.”
Hayo ni ya kabla ya kampeni na uchaguzi. Baada ya uchaguzi mtandao uliendelea na kazi yake. Baada tu ya uchaguzi wa 2010 na Samwel Sitta kupigwa dafrau uspika kitendo kilichomfanya kuanza kuwalalamikia wenzake kwamba ni mafisadi ndo wamemwangusha, gazeti moja linalomilikiwa na kada maarufu wa CCM, lilidiriki kutamka kwamba ugomvi wa Sitta na anaowaita mafisadi unatokana na kunyimwa uwaziri mkuu mwaka 2005.
Kwa hiyo baada ya uchaguzi 2005 mtandao ulifanya kazi nyingine haramu ya kugawa vyeo kwa walioshiriki tendo haramu la kumwingiza Kikwete madarakani kwa nguvu. Na hapo hapo wakiwabadilishia wengine vyeo walivyoahidiwa huku wakiwanyima wengine vyeo walivyoahidiwa.
Kitu hicho kilisababisha mgawanyiko na chuki miongoni mwao na mtandao kuvunjika na kuundwa mitandao mingine kadhaa kuelekea 2015. Ni hiyo ambayo sasa inakiumiza sana chama chake. Lakini si hivyo tu, wana CCM walianza kujifunza kwamba kumbe ukitaka kupata uongozi unaoutamani, unda mtandao.
Tafuta fedha nyingi, honga watu: wanachama, viongozi, wanahabari na hatimaye wananchi. Utapata kura za asilimia 80 na kuendelea. Kama huna pesa usijali. Ili mradi una nafasi ama mzazi wako ama ndugu yako ana nafasi ya kushika mali ya umma, pora hiyo mali ya umma maana haina mwenyewe uitumie kujiwekea mazingira mazuri mbele ya safari.
Inashangaza leo Kikwete anazungumza akijidai anazungumza kwa uchungu sana. Waandishi na wachambuzi mbalimbali tulimwambia. Tulimweleza kwamba alichoanzisha ni sawa na ‘kula nyama ya mtu’. Si yeye wala wenzake ndani ya chama watakaoacha. Wote wataendelea na dhambi hiyo na chama kitakufa kikiwa kimeshaidhoofisha sana nchi!
Si siri hata CHADEMA wakiingia madarakani 2015 watahitaji kufanya kazi ya ziada kuirudisha nchi kwanza kwenye pointi sifuri ya maendeleo maana kwa sasa iko hasi kabisa kutokana na matendo haya ya akina Kikwete.
Tulimwambia avunje kundi lake na kila aliyekuwa ndani ya kundi ambaye badala ya kufanya siasa za kistaarabu za kujenga hoja alijiingiza katika rushwa na matumizi mabaya ya vyombo vya habari na kibaya zaidi kupora mali ya umma, apelekwe mahakamani.
Kwa kuwa alijua akiwapeleka mahakamani waliopora pesa za EPA watamtaja na yeye, akaamua kuweka pamba masikioni.
Ndiyo maana nilifikia mahali nikakubali kwamba Kikwete ni Chaguo la Mungu. Katumwa na Mungu kuiua CCM kwa maslahi ya taifa. Rais wangu na mwenyekiti wa chama kikongwe, usilie. Kuutoa mwiba kwenye mwili lazima kulete maumivu makali. Vumilia! CCM inajimaliza mbele ya Watanzania.
Itatolewa kwenye uongozi kama mwiba utolewavyo mwilini. Subiri ikishapigwa chini, ustaafu na kuwaachia akina Nape kama wanaweza waijenge upya itarudi madarakani kama wananchi wataona kweli imebadilika. Maneno ya “chama kitafika pabaya” ni ya kuwapaka wanachama mafuta kwa mgongo wa chupa. Waeleze wazi tu kwamba chama kimeshafika pabaya na kiukweli 2015 kinang’oka madarakani. Kwa kuwaeleza ukweli, watajiandaa
kalamu ya mwigamba-Tanzania daima

No comments:

Post a Comment