Wednesday, October 31, 2012

Hotuba ya Mbunge wa Chadema yamkuna Rais Kikwete (JK)

HOTUBA ya Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema) akisifu utendaji kazi wa Rais Jakaya Kikwete na kwamba wananchi wa Rombo wana imani naye kubwa jana ilimkuna Rais Kikwete.
Katika hotuba yake katika sherehe za uzinduzi wa Barabara ya Mkuu-Tarakea, Selasini alisema wapo wanasiasa ambao hakuwataja wenye desturi ya kupanda kwenye migongo ya mafanikio ya wenzao.
Alisema kama angekuwa na uwezo angeipa barabara hiyo jina la “barabara ya JK” kwa sababu ndiye aliyetoa fedha za ujenzi wa barabara hiyo na kuhakikisha ndoto ya wananchi wa Rombo inatimia.

“Nina kila sababu ya kukushukuru na kukupongeza kwa sababu wapo wanasiasa wamekuwa na desturi ya kupanda kwenye migongo ya wengine wamekuwa wakisema wamejenga hii barabara”alisema.

Alisema barabara hiyo imekuwa katika makabrasha tangu enzi za ukoloni. lakini ni Rais Kikwete ambaye ametimiza ndoto ya Warombo ya kuungana tena na wenzao kwa shughuli za kibiashara.

Selasini alisema Wananchi wa Rombo walikuwa kama wametengwa na wananzi wenzao wa wilaya nyingine kwa vile walikuwa wakitumia siku zaidi ya saba kutoka Tarakea hadi Moshi mjini.

Mbunge huyo alimuomba Rais Kikwete asaidie kujenga malambo mawili kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na pia kikosi cha kudhibiti tembo kutoka Kenya kipatiwe gari la doria.
Alisema Rais Kikwete ndiye aliyetoa ahadi ya kuijenga barabara hiyo ambayo huko nyuma iliwahi kutolewa ahadi nyingi za kujengwa lakini hazikuweza kutekelezwa hadi Rais Kikwete alipoivalia njuga.
Kwa mujibu wa Selasini,wananchi wake wana imani kubwa na utendaji wa Rais Kikwete katika kipindi cha miaka mitatu iliyobaki na akasema kwa ujenzi wa barabara hiyo kamwe hawatamsahau maishani.

Katika hotuba yake, Rais Kikwete alisema Selasini ni mfano mwema wa siasa na akasema anaposemea mahitaji ya Wananchi wa Rombo anaiambia Serikali na kuahidi kutekeleza ombi lake la malambo.
“Nakushukuru kwa maneno yako mazuri wewe ni mfano mwema wa siasa za vyama vingi, hakuna neno zuri bali kuna wanaotawala na wako wanaopika utawala”,alisema Rais Kikwete bila kufafanua.

Alisema haitakuwa na maana kwamba kila kizuri kinachofanywa na Serikali basi viongozi wa upinzani wakibeze akisema angeshangaa kama wapinzani watakataa hajajenga barabara hiyo

Rais Kikwete alisema kuzinduliwa kwa barabara hiyo iliyojengwa kwa usimamizi wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), kutafungua fursa za kiuchumi kwa wananchi wa Rombo na nchi jirani.

No comments:

Post a Comment