Thursday, October 25, 2012

MADIWANI wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), katika Manispaa ya Moshi, Kilimanjaro juzi walitwangana makonde,Mwenyekiti Chadema achomwa mkuki

MADIWANI wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), katika Manispaa ya Moshi, Kilimanjaro juzi walitwangana makonde huku kiini kikitajwa kuwa ni gari la Mstahiki Meya.
Tukio hilo linadaiwa kutokea juzi katika moja ya kumbi za mikutano ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi wakati madiwani hao wakiwa katika kikao cha ndani cha maandalizi ya mkutano wa baraza la madiwani.
Hata hivyo, licha ya taarifa za tukio hilo kuzagaa haraka, wahusika wameifanya siri ili kulinda heshima ya chama hicho.
Inadaiwa kuwa kisa cha kupigana ni ubishi juu ya nani anastahili kupanda gari hilo la Meya na baada ya kurushiana maneno, madiwani hao walivaana na kuanza kupigana kabla ya kuamuliwa na wenzao.
Habari zinadai kuwa madiwani watatu wamekuwa wakilitumia gari la Meya kila wanapolihitaji bila kikwazo jambo ambalo limekuwa likiwakera baadhi yao.
Mwenyekiti wa Madiwani wa CCM katika Baraza hilo, Michael Mwita amekiri kuarifiwa juu ya tukio hilo lakini hakulishuhudia akisema alikuwa katika ukumbi mwingine.
Meya wa Manispaa ya Moshi, Jaffar Michael hakupatikana kuzungumzia tukio hilo kwani tangu juzi, simu yake imekuwa ikiita bila kupokewa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, Bernadette Kinabo alisema amesikia kutokea kwa tukio hilo.
Alisema tukio hilo limemsikitisha na kuwataka madiwani kuhimili jambo hata kama ni kutukanwa... “Nimearifiwa juu ya jambo hilo japo si kwa undani sana. Ila kwa kweli madiwani wanapaswa kujiheshimu ili na wengine wajifunze kutoka kwao. Haipendezi madiwani kutumia lugha ya kuudhi zaidi yao na anayetolewa lugha hiyo naye lazima azuie jazba.”


Mwenyekiti Chadema achomwa mkuki

Mwenyekiti wa Chadema, Tawi la Mwawaza, Shinyanga, Bundala Katunge amechomwa mkuki baada ya kuvamiwa na
kushambuliwa na kundi la watu zaidi ya 30.
Tukio hilo lilitokea juzi katika Kijiji cha Mwawaza saa tano usiku akiwa amelala nyumbani kwake.
Mashuhuda wa tukio hilo walidai kuwa Katunge alijeruhiwa baada ya kutoka nje ya nyumba yake mara baada ya kusikia bendera ya Chadema ikishushwa kwenye mlingoti.
Ilidaiwa kuwa alijaribu kuwazuia lakini walimzidi nguvu na kuanza kumshambulia. Aliwaponyoka na kuanza kukimbia ndipo mmojawao alipomrushia mkuki na kumchoma sehemu za mbavu upande wa kushoto. Baada ya tukio hilo  kundi hilo lilitoweka.
Katibu wa Chadema Wilaya ya Shinyanga, Nyangaki Shilungushela alisema Katunge alikimbilia kwa majirani ambao walimpeleka katika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ambako alifanyiwa upasuaji na kulazwa akisema hali yake ni mbaya.
Mganga Mfawidhi Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Frederick Mlekwa alikiri kuwapo kwa mgonjwa huyo na kusema anaendelea kupatiwa matibabu.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Evarist Mangala alisema hana taarifa ya tukio hilo.
Hata hivyo, wananchi wa eneo hilo walisema jana kwamba tangu tukio hilo lilipotokea, hawajaona polisi aliyefuatilia licha ya kutoa taarifa na kupewa fomu namba tatu iliyowezesha matibabu ya kiongozi huyo wa Chadema.
“Tunashangaa ni kwa nini polisi hawajatoa ushirikiano na huku taarifa wameshazipata,” alisema mmoja wa wakazi wa kijiji hicho ambaye hakutaka jina lake litajwe.
CHANZO GAZETI  LA MWANANCHI

No comments:

Post a Comment