Thursday, October 25, 2012

SASA ni dhahiri kwamba matokeo ya uchaguzi wa UVCCM, yameigawa jumuiya hiyo,Kifo alichotabiri J.K chanukia.

ZAIDI YA 300 WASAINI KUPINGA MATOKEO,MAKONDA ANENA, AAPA KUTORUDI NYUMA
SASA ni dhahiri kwamba matokeo ya uchaguzi wa Jumuiya ya Vijana ya Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), yameigawa jumuiya hiyo na huenda ikajikuta kwenye mgogoro mkubwa wa kiuongozi ikiwa hatua za haraka hazitachukuliwa.
Hali hiyo inatazamwa na baadhi ya wachunguzi wa mambo kwamba ni kutimia kwa utabiri wa Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete ambao aliutoa wakati akifungua mkutano huo kwamba lazima viongozi watakaochaguliwa wachukue hatua za kuondoa nyufa zitakazotokana na uchaguzi huo.
Kadhalika, Rais Kikwete aliwaambia UVCCM kwamba watajuta ikiwa watachagua viongozi wasio na uwezo kutokana na kushawishiwa na rushwa, kauli ambayo hata hivyo, vijana hao waliipuuza kwani uchaguzi huo ulidaiwa kugubikwa na vitendo hivyo hali iliyozua malalamiko kutoka kwa baadhi ya wajumbe wa mkutano.
Wasiwasi wa kupasuka kwa UVCCM unatokana na wanaodaiwa kuwa wanachama wa jumuiya hiyo 379 wengi wakiwa wajumbe wa mkutano mkuu, kusaini tamko la kupinga matokeo ya uchaguzi yaliyompa ushindi wa nafasi ya mwenyekiti, Mbunge wa Donge, Sadifa Juma Khamisi na Makamu wake Mboni Mhita.
Kadhalika, hofu ya kukua kwa ufa huo, inatokana na ukimya wa aliyekuwa mgombea wa nafasi ya Makamu Mwenyekiti, Paul Makonda juu ya nafasi ya kuteuliwa kwake na Sadifa kuwa mjumbe wa Baraza Kuu la UVCCM.
Tofauti na mgombea mwenzake, Rashid Simai Msaraka aliyekubali uteuzi uliofanywa na Sadifa kumpa ujumbe wa baraza, Makonda hadi sasa hajaukubali wala kuukataa, ukimya unaotafsiriwa kuwa unaweza kuwa na ajenda kubwa ndani yake.
Hata hivyo, Makonda alipozungumza na Mwananchi jana alisema atatoa uamuzi wake baadaye pale atakapozungumza na vyombo vya habari kuhusu yaliyojiri katika uchaguzi wa UVCCM.
“Kwa sasa siwezi kusema nimekubali uteuzi huu au hapana, ninafanya hivi kwa sababu kama ulinisikia jana (juzi) nilisema uongozi tuliouchagua ni aina ya jumuiya tunayoitaka, sasa ni aina gani hiyo, nitazungumza na baada ya hapo nitatoa sababu za kukubali au kukataa uteuzi wa Sadifa,”alisema Makonda na kuongeza:
“Leo hii nikisema nakubali uteuzi huo, basi wapo watakaosema nimehongwa au nimerubuniwa, lakini pia nikisema naukataa wapo watakaosema nina uchungu wa kukosa uongozi, sasa subiri tu siku nikisema nakubali au nakataa nitatoa sababu”.
Gazeti hili jana lilipomtaka Makonda atoe ufafanuzi wa kauli yake aliyoitoa juzi alisema: “Unawezaje kujivuna kwamba wewe ni mshindi wakati dhamiri yako ikijua kwamba ulitumia hila, fedha na ulaghai, huwezi kuwa na confidence (kujiamini) hata kidogo, sasa mtu asiyejiamini hiyo ni fedheha.”

Kwa upande mwingine, kundi la vijana wanaoongoza harakati za kutaka matokeo hayo yatenguliwe, jana liliwasilisha Makao Makuu ya CCM mjini Dodoma, baadhi ya vielelezo kuhusu kuwapo kwa vitendo vya rushwa katika uchaguzi huo.
Taarifa zinasema  kundi hilo linaanda barua na kiambatanisho cha majina na saini za wanachama wa UVCCM 379 ambao mpaka sasa wamesaini tamko la kupinga matokeo ya uchaguzi huo kupeleka kwa uongozi wa CCM.
Mmoja wa maofisa wa CCM makao makuu mjini Dodoma ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe aliliambia gazeti hili kuwa: “Ni kweli wale vijana wameleta sehemu ya ushahidi wao na tumeupokea, ila tumewaelekeza kwamba lazima waandike barua ya malalamiko na iwe imefika sehemu husika katika muda wa siku 14 tangu kutangazwa kwa matokeo”.
chanzo -gazeti la mwananchi

No comments:

Post a Comment