Tuesday, October 16, 2012

Hii Makala ni kwa wanawake wotw Duniani fuatana na mwandishi Happiness Mnale-Twende kumkomboa mwanamke kiuchumi

WANAWAKE ni kundi la kijinsia ambalo limewekwa pembeni kutokana na mila na desturi potofu, mifumo dume, mifumo kandamizi na mifumo ya kinyonyaji ikiwemo ubeberu, hii imesababisha wanawake kudharaulika na kutoheshimika, kuanzia ngazi ya familia hadi ile ya jamii.
Kutokana na hali hiyo, wanawake wengi wameanza kufanya harakati ili kupinga ukandamizaji dhidi yao kwa kufanya mambo mbalimbali yanayowaonesha kuwa wao si dhaifu kama ambavyo baadhi ya jamii imekuwa ikiwachukulia.
Leo wanawake wameingia katika sekta zote za kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiteknolojia ili kuhakikisha wanapata haki zao lakini bado zipo changamoto nyingi zinazowakabili katika kutokomeza fikra potofu dhidi yao hususan wanawake walioko pembezoni.
Katika hali ya kawaida idadi kubwa ya wanawake bado wanaishi katika mazingira magumu licha ya wanawake wachache kufanikiwa na kufikia katika nafasi za juu kabisa, wao wamebakia kuwa mfano wa kuigwa na chachu kubwa kwa wanawake wengine nchini.
Kuna kauli nyingi huwa zinaelezea umuhimu wa wanawake ama mama zetu, wapo wanaosema “nani kama mama”, “ maendeleo ya jamii yanatazamwa kwa mwanamke” “kila mafanikio ya mwanaume nyuma kuna mwanamke” na kauli nyingine nyingi sana.
Kwa kweli wao ndiyo chimbuko la asilimia kubwa ya watu maarufu na wa kuheshimika kwa jinsi walivyoweza kuwaunda kimaadili na mienendo. Mifano ni mingi katika hili kama Mwl. Nyerere jinsi alivyokuwa na ukaribu na mama yake, mwanaharakati Martin Luther King Jr wa Marekani na wengine wengi.
Katika Afrika wanawake wamekuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi sana katika maisha yao kwa ujumla. Baadhi ya changamoto hizo ni za kiasili na nyingine huibuka kutoka katika makundi yanayowazunguka, mathalani wanaume.
Wengi wana mtazamo kwamba wanawake ni viumbe dhaifu, lakini kihalisia si kama wanavyodhani, kwani katika sehemu nyingi ndiyo washikiliao koo na familia. Huwa na upendo usioweza kupimika licha ya kuwepo wachache wenye kuwa na mapungufu.
Katika siku za hivi karibuni wanawake wengi wamezidi kujishughulisha katika nyanja mbalimbali za kuzalisha kipato, si kujinufaisha nafsi bali kuinua familia na kukidhi mahitaji. Katika hili wanaume asilimia kubwa huibua mzozo mkubwa sana kwa kutokuwa tayari kuwaruhusu washiriki katika shughuli za uzalishaji mali.
Wanawake wakijishughulisha katika kazi za kilimo mashambani huko vijijini huwa ni sawa machoni pa wanaume lakini si kuingilia baadhi ya shughuli mathalani biashara, hofu i wapi? Je, si moja ya shughuli za kuzalisha mali?
Wapo waliowahi kutishiwa kuachwa, kisa hawatakiwi kujishughulisha na shughuli ya aina fulani.Lakini sijawahi kusikia mwanamke anamchagulia kazi ama kumdhibiti mwanaume katika aina ya shughuli ya kuzalisha mali.
Wapo wanaoamua waingie nao katika shughuli za kuzalisha mali baada ya kuona manyanyaso yanazidi kutokana na kuwa tegemezi kwa mwanaume mzalishaji pekee. Lakini pia ni busara na wanawake kupewa ruhusa kufanya kazi kwani kazi ni kipimo cha utu, hata vitabu vya dini vinasema asiye fanya kazi na asile.
Wanaoweza kuweka uso gumegume huingia na kuanza kupambana na mifumo hasi dhidi yao katika nyanja mbalimbali ya kazi. Wapo ambao hususiwa bidhaa kisa wao ni wanawake ati hawapaswi kununua biashara zao na wanaamua kununua za wanaume tu.
Hizo ni changamoto tu wanazokutana nazo wanawake lakini japo wanakatishwa tamaa wanawake wengi hawajakata tamaa na kuamua kuanzisha vikundi mbali mbali vya maendeleo ili kujikomboa kiuchumi.
Kati ya taasisi ambazo zimepanga kujikita kumkomboa mwanamke kifikira ni Tanzania Women Entrepreneurs and Networking Development Exposition (Twende) ambayo imepanga kuleta maendeleo kwa wanawake kwa kuandaa jukwaa ambalo litakuwa mahususi kuweza kukutana zaidi ya wanawake wafanyabiashara wakubwa 100 kutoka viwanda vikubwa na vidogo, serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO).
Twende imepanga kulenga kuyapa fursa makampuni kukutana yakikidhi malengo ya wahudhuriaji ili kuonesha bidhaa na huduma za kampuni zao kwa wafanya maamuzi.
Taasisi hiyo itajumuisha na maonesho ya daraja la kwanza yenye zaidi ya washiriki 100, maonesho hayo yatakayoenda sambamba na mkutano utakaotoa elimu bora kwa washiriki.
Ikiwa imejidhatiti kwa malengo ya kuwaelimisha kuhamasisha na kuwaendeleza wanawake Tanzania. Twende imepanga kuchangia kutangaza malengo ya milenia katika lengo la 1,3,5 na 8, ambayo ni kuondoa umasikini na njaa, kutangaza haki na fursa sawa kwa wote.
Katika maonesho hayo yatakayoanza oktoba 15, mwaka huu katika viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Twende watawahamasisha wanawake kulinda afya zao na kuendeleza uhusiano wa kudumu kwa ajili ya maendeleo ya jamii, kukuza uzalishaji kwa wanawake wafanyabiashara, kukuza mgawanyiko wa masoko, kukuza muonekano wa wafanyabiashara wanawake katika jamii, kukuza muonekano na uwepo wa usawa wa biashara.
Wakiwa na dhamira ya kuendeleza na kuthamini mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa kwa kutambua uwezo na mafanikio ya wanawake wajasiriamali, ukijumuisha na wale wenye ulemavu ili kuleta ajira.
Kuonesha wanawake wajasiriamali kama mfano wa kuigwa katika maendeleo, kuongeza juhudi za maendeleo za wanawake wajasiriamali, kutoa ujumbe na kubadilishana mbinu nzuri za kibiashara, kuwajenga wafanyabiashara wanawake kwa kuanzisha saccos, kuendeleza uzalendo wa kutumia na kuthamini bidhaa za Tanzania, kutengeneza jukwaa kwa ajili ya wanawake wenye uwezo mdogo, wa kati, mkubwa na wale wa mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO).
Pia watawawezesha kuonesha bidhaa na huduma zao kwa pamoja kwenye mpangilio mzuri, kutengeneza mahusiano ya wanawake wajasiriamali kimkoa, kitaifa na kimataifa.
Kwa mantiki hiyo twende imejipanga kumkomboa mwanamke katika suala zima la uchumi ikiwamo kumpatia mbinu za kujiinua kimaisha kupitia ujasiriamali.
chanzo -Tanzania daima

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu namba 0712 00 35 39; barua pepe: mnaleh@yahoo.com

No comments:

Post a Comment