Sunday, June 9, 2013

Warioba: Ikulu kugawanywa

Dar es Salaam: Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema iwapo Mfumo wa Serikali Tatu utaridhiwa na wananchi ni lazima mambo yaliyo ndani ya Muungano yatagawanywa ikiwa ni pamoja na Ikulu ya Rais.
Amesema kuwa kutokana na taifa kufanya mabadiliko ya Katiba ni lazima kuwepo mpangilio wa kugawana mambo mbalimbali yaliyokuwa chini ya Muungano ikiwamo majengo, wafanyakazi, Ikulu, hata vitendea kazi na kwamba utaratibu huo ni kama ule uliotumika wakati Tanganyika na Zanzibar zilipoungana.
Kauli ya hiyo ya Jaji Warioba imekuja siku tatu tangu Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe kueleza kuwa Tanzania Bara itaanza mchakato wa kutunga Katiba yake Aprili mwaka 2014 na kumalizika Desemba mwaka huohuo.
Jaji Warioba aliyasema hayo katika mahojiano maalumu na waandishi waandamizi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), inayochapisha magazeti ya Mwananchi, Mwananchi Jumamosi, Mwananchi Jumapili, Mwanaspoti, The Citizen na The Citizen on Sunday, Tido Mhando ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa MCL na Theophil Makunga, Meneja wa Uendeshaji na Biashara MCL.
Swali: Makao Makuu ya Serikali ya Muungano yatakuwa wapi?
Warioba: Ukibadili Katiba wakati wowote ni lazima kuwe na makubaliano fulani.
Unajua Serikali ya Muungano na Tanganyika ilikuwa pamoja, sasa ukianzisha Serikali ya Tanganyika, lazima kwenye mpangilio muanze kugawana hata wafanyakazi kwa kuwa wafanyakazi hao walikuwa ni wa Muungano. Hapo ndiyo mtaamua wafanyakazi gani watakwenda katika Serikali ya Tanganyika, watakaobaki katika Muungano na wale watakaokwenda Zanzibar.
Hata katika majengo hali inakuwa hivyo hivyo, lazima kutakuwa na majengo yaliyokuwa yakitumiwa na wizara mbalimbali na hata Ikulu. Hapo pia lazima myagawanye na kukubaliana viongozi wa Tanganyika watakuwa wapi na wale wa Muungano watakuwa wapi. Lakini, hata vifaa vya kutendea kazi navyo inatakiwa mgawane kulingana na makubaliano yenu.
Suala hili linategemea zaidi mazungumzo ya pande zote mbili, baada ya kukamilika kwa mchakato huu kwa sababu hii iliyopatikana sasa ni rasimu tu, ambayo itajadiliwa na wananchi kabla ya kuanza kwa Bunge la Katiba na baadaye kuwepo kwa kura ya maoni. Wapo watakaokuwa wakihoji kuhusu vyeo, katika hili itakuwa kama tulivyokuwa tukiungana Tanganyika na Zanzibar, wakati huo wapo ambao walikuwa wakuu wa mikoa na wakajikuta wameingia katika Muungano huku wakiwa na vyeo hivyo. Kilichofanyika ni kuendelea tu na nafasi hizo mpaka utakapofanyika utaratibu mwingine kwa njia ya mazungumzo.
Unajua jambo hili siyo jukumu la tume hii, tunaliacha kwa sasa na hatujui litakuwaje kwa sababu ni suala la mazungumzo.
Swali: Majukumu ya Rais yatakuwaje?
Warioba: Rasimu imeeleza majukumu (roles) ya Rais kama mkuu wa nchi, ambaye anakuwa kama taasisi na sisi tulichokifanya ni kujenga taasisi hizo, kwamba ijulikane akifanya chochote awe ameshauriwa, isiwe yeye peke yake.

Msanii bongo movie aliyeanza kucheza filamu Ulaya

Kama utakuwa shabiki na mtazamaji mzuri wa filamu za bongo movie, jina la Lucy Francis Komba halitakuwa jipya masikioni mwako.
 
Msanii huyu alianza sanaa katika Kundi la Kaole, akishiriki baadhi ya vipindi vya televisheni na baadaye kujiunga na Kikundi cha Dar Talent, ambapo alishiriki filamu moja ya vichekesho.
Katika sanaa, Lucy ameshacheza filamu zaidi ya 50 zikiwemo nne alizocheza nje ya nchi. Filamu ya kwanza aliyocheza nyota huyu na kuonyesha kipaji chake inafahamika kama Utata. Baadaye alishiriki filamu ya Yolanda, Division of Love, Jeraha la Ndoa, Talaka Wodini, Siri ya Moyo Wangu, Teke la Mama, Richmond, Swadakta na nyinginezo.
Kwa sasa Lucy ni mwigizaji wa filamu, mwongozaji, mtunzi wa stori na mtayarishaji wa filamu aliyefanikiwa kuvuka mipaka ya nchi hasa Bongo Movie akichanua hadi katika nchi za Burundi, Sierra Leone na Denmark.
Lucy kwa sasa anasubiri kuzindua filamu yake mpya aliyoichezea nchini Denmark.
”Nilienda kupumzika tu, lakini baada ya kuona wana mwitikio mzuri na filamu zetu, ilinibidi nicheze filamu niliyoipa jina la ‘Tanzania to Denmark’,” anasema Lucy.
Anabainisha kuwa filamu hiyo amecheza kwa gharama zake akishirikiana na Kampuni ya Vad Production ya Denmark inayojihusisha na uzalishaji wa filamu.
“Walinisaidia sana hadi hatua ya mwisho. Natarajia kuizindua mwezi huu wa Juni nchini Denmark, naamini itauza sana, maana nimecheza na wasanii maarufu wa huko,”anasema Lucy.
Aprili mwaka jana, msanii huyo alifanikiwa kwenda nchini Ghana kwa maandalizi ya kucheza filamu yake, hata hivyo hakuweza kufanikiwa baada ya msanii mwenzake Kanumba kufariki dunia.
“Mimi nilikuwa nimeshatangulia, nikiwa huko nikasikia amefariki ikanibidi nirudi kwanza nyumbani kwa mazishi yake,”anasema Lucy.
Kabla ya kuondoka Ghana, Lucy alibahatika kufanya mahojiano na mastaa wa nchini Sierra Leone waliokuwa wakikusanya washiriki wakubwa kwa lengo la kuandaa filamu itakayojitambulisha kimataifa.
Maandalizi hayo ni maarufu kama ‘famous film magazine in Africa’ ambayo imewashirikisha baadhi ya nyota akiwamo Van Vicker, Ini Edo, Desmond na wengineo katika kuandaa filamu ya ‘Repackage live’.