Tuesday, October 9, 2012

Wabunge Kenya wataka kulipwa mamilioni,wawafunika wabunge wa Tanzania

                                             Kero la wananchi wa Kenya kwa wabunge wao
Waandamanaji waliojawa na ghadhabu nchini Kenya wamejitokeza kulaani hatua ya wabunge nchini humo kutaka kujilipa mamilioni ya pesa kama pesa za ziada wakati bunge litakapofunga vikao vyake kwa maandalizi ya uchaguzi mwaka ujao.
Wabunge hao ni baadhi ya wale wanaopokea mishahara mikubwa sana barani Afrika , wakipokea takriban dola elfu 10,000.
Malipo hayo ya ziada ya dola 105,000 kwa kila mmoja yatalipwa wakati wabunge watakapofunga vikao vyao kwa maandalizi ya uchaguzi mkuu mwaka 2013.
Wadadisi wanasema kuwa huenda wananchi wakatozwa kodi zaidi ili kugharamia malipo hayo ya dola milioni 23.
Hatua hii imewakasirisha watu wengi, hasa ikizingatiwa kuwa inakuja baada tu ya migomo katika sekta ya umma ambapo madaktari, walimu na hata wahadhiri wa vyuo vikuu walisusia kazi wakidai nyongeza ya mishahara.
Mswaada huo ulipitishwa siku ya Alhamisi ikiwa sehemu ya mabadiliko yaliyofanyiwa sheria ya fedha bungeni.
Mnamo mwezi Septemba, shule za umma zilifungwa kwa wiki tatu wakati walimu walipogoma wakidai nyongeza ya mishahara na huku madaktari nao wakitaka mazingira bora ya kazi.

No comments:

Post a Comment