Tuesday, October 30, 2012

JESHI la Polisi Mkoa wa Arusha, limemsafisha Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari

JESHI la Polisi Mkoa wa Arusha, limemsafisha Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (CHADEMA), kuwa hakuhusika katika tukio la kufyatua risasi hewani kama ilivyodaiwa na baadhi ya vyombo vya habari jana.
Badala yake, Kamanda wa Polisi Mkoa, Liberatus Sabas, alisema kuwa wanamhoji mjumbe wa mkutano Muu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kupitia Wilaya ya Arusha, Godfrey Mwalusamba, kuhusiana na tukio hilo.
Kufuatia hatua hiyo, Nassari ametoa siku 14 kwa magazeti ya Uhuru na Habari Leo kukanusha taarifa walizoandika wakimhusisha na tukio hilo kwenye Kata ya Daraja Mbili siku ya Jumapili, vinginevyo atayashitaki Baraza la Habari nchini (MCT).
Katika mkutano wake na waandishi wa habari, Kamanda Sabas alisema kuwa Mwalusamba alifyatua risasi hewani kwa lengo la kumuokoa mwanamke mmoja ambaye jina lake hakulitaja, ambaye alikuwa akishambuliwa na kundi la vijana wakimtuhumu kuwa alikuwa akigawa fedha kwa wapiga kura.
Alisema kuwa kwenye tukio hilo, Musa Khamisi, alijeruhiwa kwa kukatwa na panga ambapo jumla ya watu wanane walikamatwa na tayari walifikishwa mahakamani jana kujibu mashitaka ya kujeruhi na shambulio la aibu.
Naye Nassari, aliwaambia waandishi wa habari kuwa amefikia uamuzi wa kuyataka magazeti hayo kukanusha habari hizo kwa uzito uleule waliotumia kuzitangaza baada ya kutafakari na kujiridhisha kuwa habari hizo ziliandikwa kwa hila, zikiwa na lengo la kumchafua.
“Magazeti hayo yameandika kuwa nilifyatua risasi saa saba mchana Kata ya Daraja Mbili wakati muda huo nilikuwa Kata ya Bangata nikiwa wakala mkuu wa uchaguzi, siku hiyo nilipita Kata ya Daraja Mbili saa mbili asubuhi kwa ajili ya kushusha mawakala kisha nikaondoka,” alisema.
Alisema kuwa habari hiyo iliyoandikwa na gazeti la CCM na lile la Serikali iliandikwa kimkakati kwa lengo la kumchafua yeye binafsi na chama chake huku akiweka bayana kuwa huo ni mwendelezo wa hila anazofanyiwa tangu anyakue ushindi wa jimbo hilo.
source-tanzania daima

No comments:

Post a Comment