Monday, October 8, 2012

Hugo Chavez ashinda muhula wa 4,Je siri ni nini?

                                                                 Rais Hugo Chavez
Rais wa Venezuela Hugo Chavez ameshinda muhula wa nne mamlakani baada ya mgombea wa upinzani Henrique Capriles kukubali kushindwa katika uchaguzi uliofanyika siku ya Jumapili.
Bwana Chavez alishinda uchaguzi huo kwa asilimia 54.
Bwana Chavez, alisema ataendelea kuhakikisha kuwa nchi hiyo imevuna matunda ya ujamaa na pia akaahidi kuwa atajikakamua kuwa rais mzuri.
Rais wa tume ya uchgauzi Tibisay Lucena alitangaza kuwa asilimia 90 ya kura zilizohesabiwa bwana Chavez alishinda asilimia 54.42 huku mpinzani wake akichukua asilimia 44.97.
''Utawala wa mapinduzi umeshinda" bwana Chavez aliwaambia wafuasi wake waliokuwa wanamshangilia sana katika ikulu ya Rais.
"Viva Venezuela! Viva the fatherland! Alisema bwana Chavez. Kinyang'anyiro kilikuwa kikali na ushindi uko sawa.
Hata hivyo, Chavez pia alisikika akitoa kauli ya kusema kuwa serikali yake itawajumuisha kila mwenye maono sawa na yeye. ''Ninajitolea kuwa rais bora kuliko nilivyokuwa katika siku za nyuma'' aliahidi Rais Chavez.
Mgombea mwenzake, bwana Capriles alimsifu na kumpongeza Chavez, na kuwaambia wafuasi wake wasihisi kama wameshindwa.
"nataka kumpongeza mgombea mwenzangu, rais wa nchi yetu'' alisema akiwa katika makao makuu ya kampeni yake.
Aliongeza kuwa "tumepanda mbegu nyingi,kote nchini Venezuela na ninajua mbegu hizi zitazaa miti mingi''
Wafuasi wa Chavez waliojaa furaha, walisherehekea katika barabara za mji mkuu wakipeperusha bendera.
Kwa upande wake, Henrique Capriles, alikubali kushindwa na kuwataka wafuasi wake kutovunjika moyo.
Watu nchini humo wamepokea ushindi wa Chavez kwa hisia mbali mbali. Edgar Gonzalez ambaye ni mfanyakazi wa ujenzi, alisema '' siamini , nina furaha nyingi sana ''
Rais Chavez ni mmoja wa wakosoaji wakubwa wa Marekani kutoka Amerika ya Kusini. Mshindani wake alimtaka afahamu kuwa nusu ya watu nchini humo wanaotofautiana na sera zake. Bwana Chavez aliugua maradhi ya saratani na kutibiwa nchini Venezuela ingawa sasa hana tena maradhi hayo.

No comments:

Post a Comment