Friday, December 28, 2012

Msigwa: CCM mnapoteza muda Iringa

MWENYEKITI wa Chadema Mkoa wa Iringa Mchungaji Peter Msigwa ameponda mikakati iliyotangazwa na viongozi wa (CCM) wa Mkoa wa Iringa ya kutangaza dhamira ya kurejesha jimbo hilo mikononi mwa chama hicho akisema kitendo hicho si utatuzi wa kero za wakazi wa Mkoa wa Iringa.
Msigwa alihoji ikiwa chama hicho tawala kitafanikiwa kurejesha jimbo lilikuwa likishikiliwa na CCM kwa miaka mingi kabla ya wananchi kuchagua upinzani mwaka 2010 kama ndiyo njia ya utatuzi wa kero za wananchi.

Akizungumza na gazeti hili alisema anashangazwa na mawazo ya viongozi hao wanaofikiria leo kurejesha jimbo badala ya kushugulikia kero za wananchi ambazo alisema zinakwamishwa na utendaji mbovu wa Serikali ya CCM.

“Leo Iringa gunia mmoja la Mahindi Sh80,000, wananchi wa kipato cha chini hawana uwezo wa kununua, yote haya ni matokea ya Serikali ya CCM ya kushindwa kusimamia na kujali wananchi wake, ikiwa watachukua jimbo hili wanataka kusema ndilo litakuwa suluhisho la migogoro na kero za wakazi wa Iringa mjini?,” alihoji Msigwa na kuongeza:

“Hadi sasa ndani ya CCM hakuna mgombea anayeweza kusimama na kupambana na nguvu ya umma katika jimbo hilo na si lazima nipitishwe mimi na chama changu kugombea bali mtu yeyote atakayeteuliwa wananchi watamchagua ili mradi atapitishwa na Chadema” alisema.

Msigwa ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini alitoa kauli hiyo jana kufuatia viongozi wa CCM wa Mkoa wa Iringa wakiwa ni wa chama na jumuiya zao kueleza mikakati waliyonayo kuwa ni pamoja na kurejesha Jimbo hilo mikononi mwa chama chao.

No comments:

Post a Comment