Saturday, December 15, 2012

Chadema kujadili mpasuko

KAMATI Kuu ya Chadema imekutana Dar es Salaam jana katika kikao chake cha siku mbili ambacho  pamoja na mambo mengine, kinatarajiwa kuutafutia dawa mpasuko mkubwa ndani ya chama hicho mkoani Arusha kwa kuwajadili viongozi wa chama hicho Jimbo la Karatu.
 
Kikao hicho kilichoanza jana katika Hotel ya Blue Pearl, kinatarajia kuendelea leo na Mbunge wa Karatu, Mchungaji Israel Natse, Mbunge wa Viti Maalumu, Cecilia Pareso, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Karatu, Lazaro Maasai na Diwani wa Karatu Mjini, Jubiless Mnyenye watahojiwa.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho zilieleza jana kuwa wabunge pamoja na viongozi wa Chadema wa jimbo hilo hawaelewani na ndiyo chanzo cha kukwama kwa miradi mingi ya maendeleo, ukiwamo wa Maji Karatu Vijijini (Kaviwatu).
Kikao cha dharura cha Kamati Kuu kilichokaa Septemba 9 mwaka huu, kiliunda Tume ndogo ya kuchunguza suala hilo ambayo ilipendekeza baadhi ya madiwani kuchukuliwa hatua.
Katika kikao cha jana, ajenda kuu zilizokuwa zikijadiliwa ni taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya kikao cha dharura cha Septemba 9, mwaka huu.
Katika kikao hicho mbali ya kuagiza chama kimwandikie barua rasmi Rais Jakaya Kikwete ili asimamie utekelezaji wa baadhi ya masuala yaliyoko kwenye mamlaka yake kwa mujibu wa Katiba ya Nchi, pia kiliazimia masuala kadhaa.
Mambo hayo ni pamoja na kuwataka Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi, Mkuu wa Jeshi la Polisi Inspekta Jenerali, Said Mwema, Mkuu wa Operesheni wa Jeshi la Polisi, Kamishna Paul Chagonja na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, wawajibike kwa kujiuzulu nafasi zao au wafukuzwe kazi.
Pia kiliazimia kwamba Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda, Mkuu wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mkoa wa Morogoro na askari waliosababisha mauaji ya raia wasio na hatia Morogoro na Iringa wafikishwe mahakamani kujibu mashtaka ya mauaji.
Mbali na kupokea taarifa hiyo kikao hicho pia kilijadili hali ya kisiasa nchini, mchakato wa Mabadiliko ya Katiba ya nchi na Operesheni ya Vuguvugu la Mabadiliko (M4C).
Bavicha wakana
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha), Mkoa wa Mwanza, Liberatus  Mulebele amesema hakuna vijana wa chama hicho ambao wamemkataa Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Mulebele amesema yeye ndiye msemaji mkuu wa masuala yote yanayohusu Bavicha kwa Mkoa wa Mwanza na kwamba hakuna mtu mwingine.
“Kwa mamlaka yangu ninaelewa fika vijana wa Mwanza hawajawahi, wala hawana mpango wa kubeba propaganda za CCM dhidi ya Chadema na viongozi wetu kuanzia ngazi ya chini hadi ya juu, akiwamo Katibu Mkuu, Dk Slaa,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Kiongozi huyo amesema vijana wa Chadema Mkoa wa Mwanza wako pamoja akisema waliotoa taarifa za kumtuhumu Dk Slaa si wenzao.

No comments:

Post a Comment