Wednesday, December 12, 2012

Nyalandu ageuziwa kibao kuhusu rushwa Tanapa

SAKATA la Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu kudaiwa kuingilia utendaji wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) kwa masilahi yake binafsi limezidi kuchukua sura mpya.
Safari hii, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli ameilipua Kampuni ya Ahsante Tours ambayo Waziri Nyalandu anadaiwa kuikingia kifua.
 

Lembeli ambaye pia ni Mbunge wa Kahama (CCM), aliilipua kampuni hiyo mbele ya Waziri wa Utalii, Balozi, Khamisi Kagasheki na kudai kuwa kampuni hiyo imekubuhu kwa kupitisha wageni kinyemela.

“Hii kampuni ndio notorious(imekubuhu) kwa kuiba njia… wanaoingiza watu kinyemela huko ndani na Tour Operators (kampuni)zingine zinafahamu”alisema Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Bunge.

Lembeli alisema kampuni nyingine za utalii zinalalamika kuwa Ahsante Tours ambayo imekuwa ni utaratibu wake wa kuiba njia na kuikosesha mapato Serikali ndio wanapewa upendeleo.

“Wenzao wanaituhumu hii kampuni kuwa ni bingwa wa kuiba njia sasa wamebanwa ndiyo hayo yameanza kujitokeza”alisema Lembeli, kauli ambayo ilionekana kumshtua Waziri Kagasheki. Waziri Kagasheki alimgeukia Mkurugenzi Mkuu wa Tanapa, Allan Kijazi na kumuuliza kama shirika lina taarifa hizo na kukiri kuwa ni kweli tuhuma hizo zipo na zinatolewa na kampuni washindani.

“Kama ni kweli basi tuachane na kampuni hii” alisema Waziri Kagasheki na kusema suala la kupitisha watalii katika hifadhi mbalimbali nchini ni kinyume cha sheria na kanuni zilizoanzisha Tanapa.

Kauli hizo za Waziri Kagasheki, Lembeli na Kijazi zilitokana na maswali ya waandishi wa habari waliohoji Kampuni ya Ahsante Tours iliwezaje kuikopa Tanapa wakati tayari walilipwa na wageni.

Utaratibu unataka kampuni ya utalii inayotaka kupandisha mgeni mlimani kulipia kwa kadi hiyo kupitia benki yoyote ya CRDB wakati kwa wanaotembelea mbuga za wanyama hulipia kupitia Exim.

Chini ya utaratibu huo, watalii binafsi ambao wana kadi za Visa au Master Card wanaweza kulipia ada zao moja kwa moja katika vituo vilivyopo kwenye malango ya kuingia katika hifadhi hizo.

Mgogoro huo umeibuka baada ya Tanapa kuifungia kampuni hiyo kwa udanganyifu, lakini Waziri Nyalandu akaingilia kati na kuiamuru Tanapa kukutana na Ahsante Tours na kumaliza mgogoro huo.
Kampuni hiyo ya mjini Moshi ilifungiwa baada ya kupitisha watalii katika hifadhi mbalimbali nchini bila kulipa ada na deni hilo kufikia Dola 80,000 za Marekani sawa na Sh155 milioni za Tanzania.
Lakini juzi Nyalandu aliitisha mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam akidai uamuzi wa Tanapa wa kuifungia Ahsante Tours ulikuwa ni wa dhuluma na kuituhumu Tanapa kwa rushwa.

Nyalandu alidai uamuzi huo wa Tanapa kuifungia kampuni hiyo ungeathiri mapato ya Tanapa kwa kuwa Ahsante Tours inatarajia kupata watalii 3,000 na pia imeajiri watanzania 600.
Lakini wakati Nyalandu akiituhumu Tanapa, taarifa mpya za namna anavyoingilia Tanapa zimeanza kuibuliwa ikiwamo ya kushinikiza Tanapa ikiuke maagizo yaliyopitishwa na Bunge.

Habari zinadai kuwa Bunge lilipitisha uamuzi kuwa kila mmiliki mwenye hoteli iliyopo ndani ya Hifadhi, ailipe Tanapa Dola 60 sawa na Sh99,000 za Tanzania kwa kila mgeni atakayelala hotelini.

No comments:

Post a Comment