Sunday, December 9, 2012

JK, Slaa, kuzungumzia katiba mwakani

RAIS Jakaya Kikwete, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk Willbrod Slaa na viongozi wengine wakuu wa vyama vya siasa nchini wanatarajiwa kutoa maoni yao kuhusu Katiba Mpya kuanzia Januari mwakani.
Hayo yalisema juzi Jijini hapa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alipokuwa  akizungumza na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama Wilaya ya Arusha wakati ujumbe wa tume hiyo ulipofika kujitambulisha kwa Mkuu wa Wilaya hiyo, John Mongela.
Jaji Warioba aliyeungana na ujumbe wa tume unaokusanya maoni ya wananchi mkoani Arusha tangu Novemba 19, mwaka huu, aliwataja wengine watakaopata fursa ya kutoa maoni mwakani kuwa ni viongozi wa taasisi za kidini, vyama vya wafanyakazi, asasi na taasisi za kiraia.
Kundi lingine litakalotoa maoni mwakani mara baada ya zoezi la kupata maoni ya wananchi kutoka mikoa yote 30, kukamilika Desemba 19, mwaka huu ni Baraza la Mawaziri, Makatibu Wakuu wa wizara, wakuu wa mashirika na taasisi za umma.
Mchakato wa kukusanya maoni kuhusu Katiba Mpya umegawanyika katika hatua nne ambazo ni kupata maoni ya wananchi wote kupitia mikutano ya hadhara kila mkoa, wilaya na kata unaotarajiwa kukamilika Desemba 19, mwaka huu.
Baada ya kukusanya maoni ya wananchi, Tume itaandaa rasimu ya Katiba Mpya itakayorejeshwa tena kwa wananchi ili waijadili na kuipitisha.

No comments:

Post a Comment