Wednesday, December 19, 2012

Hukumu rufaa ya Lema yaiva itasomwa kesho saa tatu

MBIVU na mbichi kuhusu hatima ya ubunge wa Godbless Lema katika Jimbo la Arusha Mjini zitajulikana kesho, wakati Mahakama ya Rufani itakapotoa uamuzi wa rufaa iliyokatwa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu iliyotengua ubunge huo.
 
Habari zilizopatikana jana kutoka mahakamani hapo zilisema kuwa jopo la majaji watatu waliosikiliza rufaa hiyo limeshakamilisha kuandika hukumu yake na kwamba itasomwa kesho kuanzia saa 3:00 asubuhi.
Lema ambaye ni kada wa Chadema, alivuliwa ubunge Aprili 5, mwaka huu katika hukumu iliyotolewa na Jaji Gabriel Rwakibalia kutokana na kesi iliyofunguliwa na makada watatu wa CCM; Mussa Mkanga, Happy Kivuyo na Agnes Mollel, wakipinga ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa 2010.
Pamoja na kumvua ubunge, Jaji huyo pia alimwagiza Msajili wa Wilaya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha kuiarifu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), kuhusu Lema kutiwa hatiani na kuhukumiwa kwa Kifungu cha 114 cha sheria ya uchaguzi ambacho kinamnyima kupiga au kupigiwa kura kwa kipindi cha miaka mitano.
Matumizi ya kifungu hicho ni miongoni mwa hoja zilizowasilishwa na Lema kupitia kwa mawakili wake akidai Jaji alikosea kwa sababu makosa yaliyomvua ubunge hayaangukii kwenye vitendo vya rushwa, kuzuia watu kupiga kura.
Jaji Rwakibarila alimvua Lema ubunge baada ya kuridhika kuwa alitumia lugha na kauli za udhalilishaji dhidi ya aliyekuwa mgombea wa CCM, Dk Batilda Burian), inayoangukia kwenye Kifungu cha 113.
Kutokana na hukumu hiyo, Lema, kupitia kwa mawakili wake Method Kimomogoro na Tundu Lissu alikata rufaa Mahakama ya Rufani, akiwasilisha hoja 18 za kuipinga.
Hukumu ya Jaji Rwakibarila pia ilipingwa na mawakili wa Serikali waliokuwa wakimwakilisha Mwanasheria Mkuu katika shauri hilo, Timon Vitalis na Juma Masanja ambao wanadai haina hadhi ya kuitwa hukumu kutokana na kujaa dosari za kisheria.
Hata hivyo, wakati Lema akikata rufaa, warufaniwa; Mkanga, Mollel na Kivuyo nao waliwasilisha rufaa kupitia kwa Mawakili wao, Alute Mughwai na Modest Akida kupinga uamuzi wa Jaji Rwakibarila kutupilia mbali baadhi ya madai yao.
Lema na mmoja wa wakili wake, Kimomogoro jana walithibitisha kwa nyakati tofauti kupokea hati za kuitwa mahakamani kusikiliza hukumu hiyo.
Taarifa kwamba hukumu itasomwa kesho zilitawala Jiji la Arusha jana na viongozi wa Chadema wakiongozwa na Katibu wa Mkoa, Amani Golugwa walionekana wakijiandaa kuelekea Dar es Salaam kusikiliza uamuzi huo.
Akizungumza kwa simu jana alasiri, Golugwa alisema ataongoza kundi la wanachama na viongozi zaidi ya 40 kutoka Arusha kwenda Dar es Salaam leo.

No comments:

Post a Comment