Tuesday, November 13, 2012

CCM WALIPUANA, WATAKA MAWAZIRI WANAOTOA SIRI ZA SERIKALI WATIMULIWE

Katika hatua nyingine, suala la ufisadi ndani ya CCM limeendelea kutikisa chama hicho, baada ya wajumbe wa mkutano mkuu kupendekeza kuwa makada wanaotuhumiwa kwa kashfa hiyo wavuliwe uanachama.

Vilevile, wanachama hao wamependekeza viongozi wanaotoa hadharani siri za Baraza la Mawaziri na kuikosoa hadharani Serikali waadhibiwe, wakieleza kuwa matendo hayo yanakiuka maadili ya kazi zao.

Wakitoa maazimio yaliyopatikana kutoka katika makundi yaliyokuwa yakijadili taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM, iliyowasilishwa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Wilson Mukama na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda juzi mchana, wajumbe hao walisema kuendelea kuwapo ndani ya chama hicho watu hao kunahatarisha usalama.

Akiwasilisha mapendekezo ya kundi la tatu, lililokuwa la Mikoa ya Dodoma, Iringa, Kilimanjaro, Tanga, Rukwa na Mjini Magharibi, Dk Damas Mkasa katika kundi lao wamependekeza makada wa CCM ambao wamekuwa wakikivuruga kwa kuendelea kupandikiza mpasuko waondoke.

“Wenye ndimi mbili wanaotengeneza migogoro ndani ya chama chetu waondolewe, ili CCM iendelee kushika hatamu ya nchi,” alisema Dk Mkasa, huku akishangiliwa na wajumbe wa mkutano ukumbi mzima.

Emmanuel Lwegenyeza akiwasilisha mapendekezo ya Mikoa ya Kigoma, Dar es Salaam, Kusini Unguja, Geita, Manyara na Shinyanga, alisema wajumbe katika kundi hilo wametaka wanachama wa CCM wanaotuhumiwa kwa kujihusisha na rushwa waondolewe.

“Wale ambao wanajihusisha na rushwa ndani ya chama wafukuzwe,” alisema.

Awali juzi jioni, wakichangia katika makundi wajumbe kutoka Mikoa ya Arusha, Tabora, Singida, Kusini Magharibi na Ruvuma, ambao walikuwa katika Ukumbi wa Kizota, kama wazee ndani ya chama hicho, walishindwa kuwadhibiti waachie ngazi na kuwakabidhi majukumu hayo vijana.

Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangala alisema, haiwezekani wazee waendelee kuitafuna nchi, huku Watanzania wakiendelea kuwa maskini.
“Haiwezekani wazee waendelee kuitafuna nchi na kujinufaisha wao wenyewe, kama wamechoka waondoke,” alisema.

Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinaeleza kuwa, mbunge huyo alishangaa kuona ndani ya chama hicho kuna makanda wanaotuhumiwa kwa ufisadi, lakini wamekuwa wakijitetea kuwa wasafi, huku wakiendelea kukigawa chama.

Mwakilishi wa kundi namba nne, Balozi Ali Mchumo alipendekeza kuwa ni wakati mwafaka kwa CCM kuwafagia watu wote ambao wamekuwa wakikihangaisha chama na kuwafanya wajumbe kuwa na makundi.

“Wanaomomonyoa chama watoswe kwa faida ya wengi, tumependekeza hata wale wanaovujisha siri za chama watoswe pia kuliko kuendelea kuwa nao,” alisema Mchumo.

Charles Mwakipesile ambaye alikuwa ni mwakilishi wa kundi namba tano alipendekeza kuwa watu wote ambao wamekuwa ni tatizo ndani ya chama waanze kwa kuonywa na wakirudia tena ndipo wafukuzwe.

Mwakipesile alisema ili chama kionekana kuwa ni bora, hakina budi kujipambanua kwa kuwafukuza pale itakapobidi wale ambao wanakipaka matope chama hicho.

No comments:

Post a Comment