Friday, November 16, 2012

Mpinzani wa Kilango ajiunga Chadema

Kasi ya walioanguka kwenye zoezi la kura za maoni ndani ya CCM kukihama chama hicho imeendelea baada ya aliyekuwa mgombea ubunge Jimbo la Same Mashariki, mkoani Kilimanjaro, Naghenjwa Kaboyoka, kujiengua na kujiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Baada ya kutangaza kuhama CCM, jana Kaboyoka, alichukua fomu ya kuwania ubunge Jimbo la Same Mashariki kwa Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Juma Iddi.
Akizungumzi uamuzi wake wa kujiengua CCM, Kaboyoka alisema ni kutokana na
utaratibu mbovu na haki kutotendeka katika zoezi zima la kura za maoni ambapo alishika nafasi ya pili baada ya Anne Kilango Malecela, ambaye ameteuliwa na CCM. Alisema misingi ya uchaguzi haikufuatwa na kwamba aliandika barua ya malalamiko kwa katibu wa CCM wilaya, mkoa na Taifa, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa, huku wakimbeba Kilango bila kuchunguza kasoro zilizolalamikiwa.
“Mfano, orodha ya wapiga kura haikuwepo na baadhi ya makatibu wa kata walikuwa na karatasi za kupigia kura ambazo zimeandikwa jina la
Kilango na ambazo baadhi zilikamatwa na kuwasilishwa kwa viongozi wa ngazi za juu, lakini hawakuchukua hatua, watu wasio wanachama walipewa kadi na kupiga kura,” alisema.
Alisema mamluki wengi wasio wanachama walipewa kadi za kupigia kura na hata wale ambao hawakuandikishwa katika daftari la wapiga kura la chama na wasio na kadi waliruhusiwa kupiga kura, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
“Nimeamua kwenda chama cha upinzani ambacho ni Chadema, nimejiridhisha kuwa kina sera nzuri na ambazo nimezipenda na zinazowafaa wananchi wa jimbo langu, na pia baada ya wananchi kuona utaratibu huo mbovu walikasirishwa na kuniomba niende chama kingine ili wanichague,” alisema Kaboyoka.
Katibu wa Chadema mkoa wa Kilimanjaro, Basil Lema, alithibitisha Kaboyoka kujiunga na chama hicho na kuchukua fomu ya kuwania ubunge katika jimbo hilo na kwamba wamempokea kwa furaha na matumaini makubwa.
“Tumefurahi, tumepata mpambanaji mwenzetu, kwa muda mrefu tangu mwaka 2000 amekuwa akiambiwa ndani ya chama hicho asubiri, kasubiri vipindi vitatu huku wakati hausubiri,” alisema na kuongeza: “Hivyo ni vyema awatumikie wananchi sasa iwapo watampa nafasi hiyo.”
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, Ali Idi, alithibitisha kutoa fomu ya kugombea ubunge kwa Kaboyoka.

No comments:

Post a Comment