Kasi ya walioanguka kwenye zoezi la kura 
za maoni ndani ya CCM kukihama chama hicho imeendelea baada ya aliyekuwa
 mgombea ubunge Jimbo la Same Mashariki, mkoani Kilimanjaro, Naghenjwa 
Kaboyoka, kujiengua na kujiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo 
(Chadema).
Baada ya kutangaza kuhama CCM, jana 
Kaboyoka, alichukua fomu ya kuwania ubunge Jimbo la Same Mashariki kwa 
Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Juma Iddi.
Akizungumzi uamuzi wake wa kujiengua CCM, Kaboyoka alisema ni kutokana na
utaratibu mbovu na haki kutotendeka 
katika zoezi zima la kura za maoni ambapo alishika nafasi ya pili baada 
ya Anne Kilango Malecela, ambaye ameteuliwa na CCM. Alisema misingi ya 
uchaguzi haikufuatwa na kwamba aliandika barua ya malalamiko kwa katibu 
wa CCM wilaya, mkoa na Taifa, lakini hakuna hatua zozote 
zilizochukuliwa, huku wakimbeba Kilango bila kuchunguza kasoro 
zilizolalamikiwa.
“Mfano, orodha ya wapiga kura haikuwepo 
na baadhi ya makatibu wa kata walikuwa na karatasi za kupigia kura 
ambazo zimeandikwa jina la
Kilango na ambazo baadhi zilikamatwa na 
kuwasilishwa kwa viongozi wa ngazi za juu, lakini hawakuchukua hatua, 
watu wasio wanachama walipewa kadi na kupiga kura,” alisema.
Alisema mamluki wengi wasio wanachama 
walipewa kadi za kupigia kura na hata wale ambao hawakuandikishwa katika
 daftari la wapiga kura la chama na wasio na kadi waliruhusiwa kupiga 
kura, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
“Nimeamua kwenda chama cha upinzani 
ambacho ni Chadema, nimejiridhisha kuwa kina sera nzuri na ambazo 
nimezipenda na zinazowafaa wananchi wa jimbo langu, na pia baada ya 
wananchi kuona utaratibu huo mbovu walikasirishwa na kuniomba niende 
chama kingine ili wanichague,” alisema Kaboyoka.
Katibu wa Chadema mkoa wa Kilimanjaro, 
Basil Lema, alithibitisha Kaboyoka kujiunga na chama hicho na kuchukua 
fomu ya kuwania ubunge katika jimbo hilo na kwamba wamempokea kwa furaha
 na matumaini makubwa.
“Tumefurahi, tumepata mpambanaji 
mwenzetu, kwa muda mrefu tangu mwaka 2000 amekuwa akiambiwa ndani ya 
chama hicho asubiri, kasubiri vipindi vitatu huku wakati hausubiri,” 
alisema na kuongeza: “Hivyo ni vyema awatumikie wananchi sasa iwapo 
watampa nafasi hiyo.”
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, Ali Idi, alithibitisha kutoa fomu ya kugombea ubunge kwa Kaboyoka.

No comments:
Post a Comment