Monday, November 26, 2012

Zitto afichua siri yake na JK

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe amefichua siri ya uhusiano wake na Rais Jakaya Kikwete kuwa, unatokana na kuheshimu mchango wake anaoutoa kwa taifa.
 
Kutokana heshima hiyo, Zitto anasema ndiyo maana Rais Kikwete hakufika jimboni kwake katika uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2005 na mwaka 2010 kumnadi mgombe wa CCM.
Zitto ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema alisema hayo katika mahojiano maalum na Mtandao wa Jamii Forum juzi.
Mbunge huyo ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, jana alilithibitishia gazeti hili kwamba alihojiwa na mtandao huo kwa saa nane.
“Kweli ni mahojiano baina yangu na Jamii Forum. Kwa Kfupi ni kwamba, yalikuwa  mahojiano ya saa nane, kuanzia saa 2 asubuhi hadi saa kumi jioni na walionihoji kwa njia ya mtandao walikuwa wakituma maswali na mimi nawajibu,” alisema Zitto.
Alisema yeye na Rais Kikwete wana uhusiano nje ya siasa na hata siku moja hawajadili mambo ya vyama vyao wanapokutana na kwamba, Rais anaamini katika uzalendo wake.
Zitto alisema kutokana Rais Kikwete kuthamini mchango wake, ndiyo maana hajawahi kwenda kwenye jimbo lake kumfanyia kampeni mgombea wa chama chake cha CCM katika chaguzi za mwaka 2005 na 2010.
“Hatuna makubaliano yeyote, bali anaheshimu mchango wangu kwenye nchi yangu. Mwaka 2005 hakuja Kigoma Kaskazini na 2010 pia hakuja Kigoma Kaskazini,” alisema.

Alisema kama ilivyo kwa wengine wenye uamuzi ya kuthamini kazi za wagombea wa vyama vingine, Rais Kikwete naye anayo haki ya kuheshimu na kuthamini kazi zake.
Aithdha, Zitto alisema anamheshimu Rais Kikwete kama mzee wake na kwamba, kuwaita kuwa wao ni marafiki ni kukosea.
“Kuita sisi ni marafiki ‘is understatement’, yeye ni mzee wangu. Tunaheshimiana, lakini ninaiheshimu zaidi Tanzania na ninaipenda zaidi Tanzania,” Zitto alisema.
Alichokifanya Rais Kikwete kutokuja katika jumbo langu si jambo geni, kwani hata vyama vingine vimewahi kuvifanya.
Alitoa mfano wa aliyekuwa mgombea wa urais kupitia Chadema katika uchaguzi mkuu mwaka 2005, Freeman Mbowe alipofika katika Jimbo la Musoma Mjini, alimpigia kampeni mgombea wa CUF.

No comments:

Post a Comment