Friday, November 30, 2012

‘Serikali imezidi kudhihirisha udhaifu’ asema Mnyika

MBUNGE wa Ubungo (Chadema), John Mnyika amesema ukiukwaji wa sheria wa matumizi ya Sh96 bilioni katika ununuzi wa mafuta mazito ya uendeshaji wa mitambo ya kufua umeme wa dharura ni matokeo ya Serikali kuwa dhaifu.
 

Amesema udhaifu huo unatokana na Serikali kushindwa kuzingatia utawala wa sheria, huku akilishukia Bunge kwamba nalo limefanya uzembe katika kusimamia utekelezwaji wa maazimio yake.

Kauli hiyo ya Mnyika ambaye ni Waziri kivuli wa Nishati na Madini imekuja siku chache tangu gazeti la East African kutoa taarifa kwamba jumla ya Dola54milioni zimegundulika kuibwa, watumishi waandamizi wa Wizara ya Nishati na Madini na Tanesco kupitia manunuzi ya mafuta ya kuendeshea mtambo wa umeme wa IPTL.

Gazeti hilo lilinukuu taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh ikieleza kuwa kuna kikundi ambacho kazi yake ni kujinufaisha na mpango huo.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Mnyika alimtaka Rais Jakaya Kikwete aagize ripoti ya CAG iwekwe wazi, kuchukuliwa hatua kwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, aliyekuwa waziri wa Wizara hiyo, William Ngeleja.

“Spika wa Bunge anatakiwa kuifuatilia wizara hii pamoja na ile ya Fedha kuhusu ufisadi huu,” ilieleza taarifa hiyo na kuongeza;
“Rais Kikwete atumie mamlaka yake kwa mujibu wa Katiba ibara za 33, 34, 35, 36 na 143 (4), aagize kuwekwa hadharani kwa ripoti ya ukaguzi maalum (Special Audit) uliofanyika mwaka 2011 kuhusu tuhuma za ufisadi na ukiukwaji wa sheria katika ununuzi wa mafuta mazito ya kufua umeme wa dharura katika mitambo ya IPTL.”

Katika taarifa hiyo Mnyika amemtaka Rais Kikwete azielekeze mamlaka na vyombo husika kumchunguza Ngeleja kwa kuwa tuhuma hizo zilitokea wakati akiwa waziri.
“Ripoti ya ukaguzi maalumu (special audit) ya mwaka 2012, ile ya uchunguzi wa Mamlaka ya Ununuzi wa Umma (PPRA) kuhusu suala hilo ziwekwe wazi” ilieleza taarifa hiyo.

Mbunge huyo alimtaka Spika Makinda naye anatakiwa kuitisha haraka kikao cha kamati mojawapo ya kudumu ya Bunge ili kuepusha udhaifu na uzembe unaoendelea kwa sasa kwa kuwa moja ya mamlaka ya Bunge ni kuisimamia Serikali.
“Juhudi hizi zinatakiwa kufanyika kwa haraka ili wizara husika itueleze kinachoendelea” ilieleza taarifa hiyo.

Mbunge huyo aliwahi kumuandikia barua Spika wa Bunge mwezi mmoja uliopita akimtaka atumie madaraka yake kukabidhi usimamizi na utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme katika moja ya Kamati za kudumu za bunge.

Inaeleza kuwa sasa anakusudia kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Spika kuhusu tuhuma za baadhi ya wabunge na na umuhimu wa hoja ya kutaka Bunge liazimie kuunda kamati Teule kuchunguza masuala yote ya ukiukwaji wa sheria, matumizi mabaya ya madaraka na tuhuma za ufisadi.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa uchunguzi huo umhusishe Mkaguzi mkuu ili kuchunguza malipo yaliyofanywa kampuni za BP (Sasa PUMA Energy), Oryx na Camel Oil ili kubaini kama kuna vigogo zaidi wa Serikali waliojinufaisha kwa kisingizio cha dharura ya umeme.

No comments:

Post a Comment