Friday, November 23, 2012

Mkewe Gbagbo kufikishwa the Haque

Simone Gbagbo
Simone Gbagbo
Mahakama ya kimataifa ya Jinai ICC, imetoa kibali cha kukamatwa kwa mke wa aliyekuwa rais wa Ivory Coast Laurent Gbagbo, Bi Simone Gbagbo.
Bi Gbagbo anasakwa kwa tuhuma za kuhusika na uhalifu wa kivita wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoibuka baada ya uchaguzi wa urais nchini humo.
Mumewe tayari amekamatwa na anasubiri kesi yake kuanza katika mahakama hiyo iliyoko The Haque, kuhusiana na madai hayo ya uhalifu wa kivita.
Takriban watu 3,000 waliuawa kwenye machafuko yaliyotokea baada ya Gbagbo kukataa kukubali matokeo ya uchaguzi wa Urais.
Gbagbo na mkewe walikamatwa ndani ya handaki moja Aprili mwaka wa 2011, miezi mitano, baada ya uchaguzi wa urais.
Wanajeshi wa rais wa sasa wakiungwa mkono na wanajeshi wa Umoja wa Mataifa walianzisha msako mkali dhidi yao, baada ya kujificha ndani ya ikulu ya rais.
Bi Gbagbo anatuhumiwa kuhusika na mauaji, ubakaji, dhuluma na ngono na kuwadhulumu wapinzani wa serikali miongoni mwa mashtaka mengine mjini Abidjan.
Licha ya kuwa Bi Gbagbo hakuwa akiwania kiti chochote cha kisiasa, ripoti zinasema kuwa alikuwa na mamlaka makubwa na kuwa alimshawishi mumeo kutokubali matokeo ya uchaguzi.
Gbagbo, 67, alihamishwa hadi The Haque mwaka uliopita na kuandikisha historia ya kuwa rais anayeondoka wa kwanza kufikishwa mbele ya mahakama hiyo ya ICC.
Rais huyo wa zamani amekanusha madai hayo yote.
Kabla ya kuhamishwa hadi the Haque, Gbagbo na mkewe mwenye umri wa miaka 63, walifunguliwa mashtaka nchini Ivory Coast, kuhusiana na uhalifu wa kiuchumi, ikiwemo madai ya kupora mali, wizi wa nguvu na kutumia rasilimali za umma kwa njia mbaya
Mahakama hiyo ya ICC sasa imetoa wito kwa serikali ya Ivory Coast, kumusafirisha Bi Gbagbo ili afunguliwe mashtaka huko the Haque.

No comments:

Post a Comment