Tuesday, January 15, 2013

UN yaunga mkono Ufaransa nchini Mali


Wanajeshi wa Ufaransa wakijiandaa kwa harakati zao nchini Mali
Wanachama wote wa Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa wameunga mkono harakati za jeshi la Ufansa dhidi ya wapiganaji wa kiisilamu nchini Mali.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon alisema kuwa anatumai hatua ya jeshi hilo itaweza kurejesha utulivu na uthabiti nchini humo.
Maelfu ya wanajeshi wa Afrika wanatarajiwa kujiunga na harakati za kijeshi dhidi ya Wapiganaji nchini Mali kusaidiana na wanajeshi wa Ufaransa.
Ufaransa iliingilia mzozo huo siku ya Ijumaa baada ya wapiganaji kuanza kusonga mbele Kusini mwa nchi.
Maafisa wa utawala nchini Ufaransa, walisema kuwa wanahofia waasi huenda wakaukaribia mji mkuu Bamako na kusababisha tisho kubwa la usalama katika eneo hilo zima.
Siku ya Jumatatu , baraza la usalama la Umoja wa Mataifa, lilifanya mkutano mjini New York kufuatia ombi la Ufaransa.
Baada ya mkutano, balozi wa Ufaransa katika Umoja wa Mataifa,Gerard Araud alisema kuwa nchi yake inaungwa mkono na wanachama wote wa baraza la usalama.
Lakini aliongeza kuwa Ufaransa pia ilitaka wanajeshi wa nchi za Afrika Magharibi kupelekwa Mali mara moja.
Hatua ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kuunga mkono jeshi la Ufaransa ni ishara ya wasiwasi mkubwa uliopo kuhusu uwezo wa makundi ya kiisilamu yaliyojihami nchini Mali.
Wanadiplomasia wanaonekana kuwa na wasiwasi kuhusu kuwasili kwa wanajeshi nchini Mali kusaidia na harakati za jeshi la Mali dhidi ya waasi.
Ramani ya Mali mpangilio wa harakati za jeshi
Huo ndio mpango wa Umoja wa Mataifa lakini azimio linalouidhinisha lilitoa muda wa mwisho mwezi mmoja uliopita kupanga harakati hizo kando na kutafuta mwafaka wa kisiasa kati ya waasi hao na serikali.

No comments:

Post a Comment