Saturday, January 5, 2013

Neno la mwisho la Sajuki

MSANII maarufu wa filamu, marehemu Sadick Juma Kilowoko maarufu kwa jina la Sajuki alitoa wasia mzito kwa wasanii siku sita kabla ya kifo chake.

Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), Simon Mwakifwamba alisema hayo jana nyumbani kwa marehemu, Tabata Bima, Dar es Salaam.
Alisema Desemba 28, mwaka huu, akiwa amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Sajuki alimweleza kuwa anahuzunishwa na ushirikiano wa wasanii nchini na kumtaka yeye (Mwakifwamba), akiwa ni  kiongozi, apeleke ujumbe huo kwao.
“Tulizungumza mambo mengi, lakini kabla sijaondoka kuna maneno ambayo ndiyo yalikuwa ya mwisho kuzungumza naye. Hayo sitayasahau kamwe. Aliniambia kwa kusisitiza zaidi ya mara mbili. Alisema wasanii wamemtupa jambo ambalo liliniumiza sana. Nakumbuka nilikwenda mimi na familia yangu kumwona hadi machozi yalinitoka.
Nilichomjibu ni kwamba binadamu akikutenga Mungu hawezi kukutenga.”
Baba mzazi wa Sajuki, Juma Kilowoko alisema familia yake imepata pigo kubwa kwani marehemu alipendwa na watu wengi kutokana na kazi yake ya kuelimisha na kuburudisha jamii.
Alisema kifo cha Sajuki kinaongeza idadi ya vifo katika familia yake kwani tayari alishafiwa na watoto wake wawili... “Sajuki ni mwanangu wa nne kati ya watoto wangu sita. Tayari nimepoteza watoto wawili.”
Kuhusu uamuzi wa kumzika Dar es Salaam, Kilowoko alisema: “Ilikuwa tumsafirishe kwenda kumzika Songea lakini kutokana na mapenzi makubwa ya wasanii wenzake na ushirikiano waliouonyesha wakati anaumwa, tumeamua kumzika hapa Dar es Salaam ili kuwapa fursa ya kumzika mwenzao.”
Viongozi  wa kisiasa jana walimiminika nyumbani kwa marehemu Sajuki. Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, Mwigulu Nchemba, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee na Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Esther Bulaya walihudhuria na kila mmoja kutoa rambirambi ya Sh1 milioni.
Kwa nyakati tofauti, Makamba na Nchemba walimwelezea Sajuki kuwa alikuwa mtu mwenye uwezo mkubwa katika kazi yake ya usanii.

No comments:

Post a Comment