Tuesday, January 15, 2013

Ndege zilizouzwa hazijulikani zilipo

WAKATI Serikali ikiwa imetenga Sh1.5 bilioni kwa ajili ya ununuzi wa ndege mpya ya Kituo cha Taifa cha Kilimoanga, pamoja na kusomesha rubani mmoja, imebainika kuwa ndege tatu za kituo hicho, zilizouzwa kwa kwa Sh500,000 hazijulikani zilipo.
Wakizungumza na gazeti hili jana kwa nyakati tofauti, Mkaguzi mkuu wa ajali za ndege nchini, John Nyamwihula na Mhandisi mkuu wa ndege wa kituo hicho, Gideon Mugusi walisema mara baada ya ndege hizo kupata ajali, Serikali ililipwa fidia na Shirika la Bima la Taifa (NIC) .
Nyamwihula ambaye alishiriki katika uchunguzi wa ndege hizo, alisema tangu NIC iilipe Serikali bima ya ndege hizo, mpaka sasa hajui ndege zilizouzwa zipo wapi.
Hata hivyo, alisema kati ya mwaka 1986 hadi 1992 kwa thamani ya Shilingi dhidi ya Dola fedha hizo zilikuwa ni nyingi ingawa zilikuwa haziwezi kununua ndege nyingine.
Alisema ndege mbili kati ya hizo ziliharibika sana, lakini moja Super Cub ilikuwa haijaharibika kwa kiwango kikubwa na ingetengenezeka lakini wakati ikirejeshwa kituoni hapo kutoka Mpanda, ndiyo ilikuwa mwanzo wa kuharibika kwake kwani ilisafirishwa kwa gari.
“Ndege hizi zilikuwa zikitumika kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao kama Quelea, Nzige, Mbung’o na wadudu waenezao Malaria,” alisema Mhandisi Mugusi.
Serikali yatenga Sh1.5 bilioni kufufua kituo
Serikali imetangaza mkakati wa kukifufua tena kituo cha Kilimoanga kwa ikiwepo kununua ndege moja, kusomesha rubani na pia kutatua matatizo kadhaa ya kituo hicho.
Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika, Christopha Chiza alisema nia ya Serikali ni kuhakikisha kituo hicho, kinafufuliwa na kufanya kazi ya kupambana na wadudu waharibifu wa mazao.
Alisema katika awamu ya kwanza, Sh1.5 bilioni zimetengwa ambazo zitatumika katika kununua ndege mpya moja na pia kugharamia mafunzo ya rubani.
Hata hivyo, wakati Serikali ikiahidi kununua ndege hiyo moja uchunguzi wa zilipo ndege zilizouzwa bado unaendelea katika wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya Uchukuzi.

No comments:

Post a Comment