Friday, January 18, 2013

Bavicha yasisitiza kumtimua Shonza

BARAZA la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), limesisitiza kuwa Juliana Shonza amevuliwa nafasi aliyokuwa akiishikilia ya umakamu mwenyekiti wa baraza hilo baada ya kukamilisha taratibu zote za kumuondoa.
 

Kauli hiyo imekuja kufuatia Shonza kunukuliwa kwenye vyombo vya habari akisema yeye bado ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza hilo kwa maelezo kuwa hakuwa amepewa barua yoyote ya kumsimamisha.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa BAVICHA, John Heche alisema Shonza alitumiwa barua ya kumvua nafasi hiyo kwa njia ya posta januari 6, hata hivyo amekuwa akikataa kuipokea.

“Lakini sio hivyo tu siku aliyokuwa anazungumza na vyombo vya habari, tulimtumia barua akakataa kuipokea, taratibu zinatuambia kumpatia barua lakini kama ameikataa bado haiwezi kubadili maamuzi ya chama,”alisema Heche.
Baada ya kumtafuta Shonza ili kutoa ufafanuzi juu ya tarifa za kupokea kwa barua hiyo zilishindikana.

Siku mbili zilizopita Shonza alikunukuliwa kwenye vyombo vya habari akisema kikao cha kamati ya utendaji cha Bavicha kilichokutana na kupitisha umamuzi wa kumfukuza kilikuwa sio halali huku akiwatupia lawama Heche na Mwenyekiti wa Chama hicho Freemon Mbowe kwa madai ya kumdhalilisha.

Shonza alisema yeye bado ni Makamu Mwenyekiti wa Bavicha na mwanachama halali wa chama hicho. Aidha alisema anafanya mkakati wa kuwashtaki wale anaowalalamikia kwa kumuita msaliti ndani ya chama hicho.

Shonza alimtuhumu Heche kutengeneza mipango ya kutukuza ukanda waziwazi ndani ya chama hicho huku akiwataka kutoa ufafanuzi wa kikatiba juu ya shutuma zinazotolewa dhidi yake.

No comments:

Post a Comment