‘Dar inachangia asilimia 80 ya mapato. Kitovu cha Uchumi. Dar inachangia 90% ya ufisadi. Uti wa mgongo wa ufisadi nchini’
Malumbano kati ya wananchi wa Mtwara na Serikali kuhusu matumizi bora
ya utajiri wa nchi yameendelea kwa takribani wiki moja sasa. Baada ya
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara na Waziri wa Nishati na Madini kuwaita Watanzania
wa Mtwara Wahaini, wapuuzi na watu hatari, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania naye aliingia kwenye mjadala huo kwa kuonya watu wanaowaunga
mkono watu wa Mtwara na kuwaita watu wanaotafuta umaarufu wa kisiasa na
wanaotaka kugawa nchi. Siku moja baada ya hotuba ya Rais, Waziri wa
Nishati na Madini alifanya mkutano na waandishi wa habari kueleza suala
lile lile ambalo bosi wake alilielezea usiku wa kuamkia mwaka mpya 2013.
Hii ni dalili ya Serikali kuweweseka.
Katika kauli ya Serikali, ambayo haikuwa na jipya zaidi ya wimbo ule
ule wa ‘kugawa nchi’ ‘umaarufu wa kisiasa’ nk, Serikali ilitaka
kuonyesha umma kuwa watu wa Mtwara hawana shukurani. Kwamba miaka yote
toka Uhuru watu wa Mtwara wamekuwa wakilishwa na Pamba, Kahawa, Chai,
Tumbaku, Sukari, Kidatu nk. Kwamba watu wa Mtwara na Lindi hawakuchangia
hata kidogo kwenye hazina ya Taifa. Hivyo wao kupigia kelele gesi yao
ni uchoyo na roho mbaya na kukosa shukurani. Kauli ya Serikali ni kauli
ya chombo kinachoendelea kukosa ‘legitimacy’ ya kuongoza taifa. Ni kauli
ya kukata tamaa. Ni kauli hatari sana dhidi ya Watanzania waliojitolea
damu kulinda uhuru wa nchi yetu.
Moja, Serikali katika kauli yake haitaji kabisa kwamba toka Uhuru
watu wa Mtwara na Lindi wamekuwa wachangiaji wakubwa sana katika uchumi
wa Taifa kupitia zao la Korosho. Takwimu za Uzalishaji wa Korosho
zinaonyesha kwamba kuanzia mwaka 1965 mpaka 2011 Korosho imeliingizia
Taifa fedha kigeni jumla ya dola za Kimarekani 4.58 bilioni ( Cashewnuts
Sub-sector study 2003, Hali ya Uchumi 2012, Cashewnuts Tanzania Report
2010). Katika Mwaka wa Uchumi unaoishia Novemba 2012, Korosho
imeliingizia Taifa jumla ya dola za Kimarekani 151 milioni. Katika mwaka
2011 zao hili liliingiza dola 130 milioni wakati Pamba iliingiza dola
53 milioni tu. Licha ya Zao la Korosho kuingiza fedha hizi za kigeni
(sawa ni shilingi trilioni 7.2) kwa nchi mikoa ya Lindi na Mtwara ipo
miaka 50 nyuma kimaendeleo kulinganisha na mikoa mingine ya Tanzania.
Serikali inataka kufuta historia ya mchango wa zao la Korosho kwenye
uchumi wa nchi yetu kwa sababu ya uroho wa gesi asilia. Kwa nini kauli
rasmi ya Serikali haijataja Korosho kabisa? Kauli hii ilipitishwa na
ngazi zote za Serikali? Mawaziri wa Serikali wanaotoka mikoa ya Lindi na
Mtwara walikubali kauli kama hii itoke dhidi ya wananchi wao
wanaoteseka na zao la Korosho miaka nenda miaka rudi?
Pili, Serikali imesahau kabisa mchango wa watu wa Lindi na Mtwara
katika ulinzi wa Taifa letu. Moja ya sababu ya mikoa ya Lindi na Mtwara
kuwa nyuma kimaendeleo ni juhudi za ukombozi wa kusini mwa Afrika. Kambi
ya wapigania uhuru wa Msumbiji ilikuwa Nachingwea. Kambi ya Frelimo
iliwekwa kwenye Shamba la Mkonge kilometa 17 tu kutoka mjini Nachingwea
ambapo ilikuwa makao makuu ya ukombozi wa Msumbiji. Rais Samora Machel,
Rais Joaqim Chissano na Rais Guebuza waliendesha mapambano kutoka kusini
mwa Tanzania. Makaburu wa Afrika Kusini na Wareno walikuwa
wanashambulia nchi yetu na mikoa hii miwili ya Lindi na Mtwara ikawa
‘buffer zone’. Wakati Dar es Salaam inaendelea kwa kila aina ya
maendeleo, mikoa ya Lindi na Mtwara ilikuwa inalinda ili wanaoishi Dar
es Salaam na mikoa mingine waishi wa amani na starehe. Serikali
inapimaje mchango huu wa mikoa hii? Tunaipima kwa fedha? Uroho wa gesi
asilia kuzalisha umeme wa kufurahisha walalaheri asilimia 14 nchini ndio
inaifanya Serikali kusahau kabisa ‘sacrifice’ ya watu wa Mtwara katika
kulinda uhuru wa Taifa letu?
Tatu, Serikali inasema lazima bomba lije Dar es Salaam kwa sababu Dar
ndio inazalisha asilimia 80 ya Mapato ya Serikali. Kwanza huu ni
uwongo. Ni aibu Serikali kujitetea kwa uwongo. Dar es Salaam ni kituo tu
cha kukusanyia mapato ya Serikali. Uzalishaji mkubwa wa nchi yetu wenye
kuzalisha kodi unafanyika nje ya Dar es Salaam. Walipa kodi wakubwa
wengi Ofisi zao Kuu zipo Dar es Salaam lakini uzalishaji wao unafanyika
nje ya Dar es Salaam. Serikali itoe orodha ya walipa kodi wakubwa 100
tuone uzalishaji halisi wa mapato hayo unafanyika wapi. Hata hivyo
inawezekana kuwa ikawa kweli Dar es Salaam inakusanya asilimia 80 ya
mapato ya nchi. Basi na tuseme Dar es Salaam inachangia asilimia 90 ya
ufisadi wote nchini. Kashfa zote kubwa za Ufisadi zinafanyika Dar es
Salaam na fedha nyingi za ufisadi zinatumika Dar es Salaam.
Mwisho, maandamano ya watu wa Mtwara ni kielelezo tosha kwamba watu
wa mikoa ya Lindi na Mtwara wamechoshwa na longolongo za Serikali.
Wananchi wa Mtwara na Lindi wanataka Uwajibikaji wa Serikali kuhusu
utajiri wa nchi. Mtanzania yeyote mwenye tahadhari ya nchi yetu kutokuwa
na laana ya rasilimali ataungana mkono na watu wa Lindi na Mtwara kudai
maendeleo. Nilitoa mfano wa Mgodi wa Golden Pride ambao umemaliza
dhahabu yote tani 76 katika eneo la Lusu wilayani Nzega. Kampuni ya
Resolute ya Australia iliwekeza dola 370 milioni kuanzia mwaka 1998
(mkataba wao ulisainiwa 25th June 1997). Katika kipindi cha uhai wa
mgodi, miaka 14, Kampuni hii imeuza dhahabu ya thamani ya dola za
kimarekani 3.3 bilioni. Kabla Serikali haijawaita watu Mtwara wahaini,
wapuuzi na watu hatari, iwaambie watu Watanzania kodi kiasi gani
imekusanywa kutoka mgodi huu katika kipindi cha miaka 14. Mpaka mwaka
2008, kwa mujibu wa Taarifa ya Kamati ya Bomani, kampuni hii ilikuwa
imelipa mrahaba wa dola 11 milioni na kodi nyingine dola 16 milioni. Serikali itwambie ilipofika Disemba 2012 kodi kiasi imekusanywa kutoka kampuni hii?
Pia watu wa Mtwara na Lindi wameona historia ya bomba la Songosongo.
Hata kodi ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (0.3%) ilikuwa inalipwa
Halmashauri ya Manispaa Ilala na kampuni ya Pan Africa Energy. Ilichukua
juhudi za mbunge wa Kilwa Kaskazini Murtaza Mangungu kuingilia kati
ndio kodi ikaanza kulipwa Kilwa ambapo uzalishaji unafanyika. Watu wa
Mtwara ni werevu, wanajua wafanyalo. Wanataka utajiri wa nchi unufaishe
nchi kwa kuanzia kule utajiri ulipo. Kuna dhambi gani?
Uwajibikaji katika uvunaji wa Rasilimali ya Gesi ndio chanzo cha
maandamano ya watu wa Mtwara. Serikali isikimbilie kulaumu wanasiasa
kwamba ndio wamechochea maandamano haya. Haya ni maandamno ya wananchi
wakitaka Serikali yao iwajibike kwao. Serikali ithubutu kufanya ubabe wa
kujenga bomba la gesi bila ridhaa ya Wananchi wa Lindi na Mtwara.
Wananchi wanapohitaji uwajibikaji ni wajibu wa Serikali kuwajibika kwao
ni sio kuwaita wahaini, wachochezi, watu hatari, wapuuzi. Watu wa Mtwara
wamechangia maendeleo ya Taifa letu kwa jasho na damu. Serikali ina
wajibu wa kuwasikiliza, kuwaelimisha na kupata mwafaka. Kauli ya
Serikali imewatukana watu wa Mtwara na Lindi. Hawatakubali
kudhalilishwa. Hawatakubali historia yao kufutwa. Hawatakubali waendelee
kubaki nyuma kimaendeleo. Serikali ifikirie tena.
No comments:
Post a Comment