Thursday, January 31, 2013

Israel yadaiwa kushambulia Syria

Urusi imekuwa ikiunga mkono sana Syria
Urusi imesema ina wasiwasi kuhusu tetesi kwamba Israel imeshambulia eneo fulani nchini Syria, ikisema kwamba shambulio hilo linakiuka Mkataba wa UN.
Jeshi la Syria lilisema mnamo Jumatano ndege za kivita za Israel zilishambulia kituo cha kijeshi cha utafiti Kaskazini-Magharibi mwa Damascus na kuwauwa watu wawili na kuwajeruhi wengine watano.
Lilikanusha habari kwamba malori yaliyokuwa yamebeba silaha na yaliyokuwa yakisafiri hadi Lebanon yalishambuliwa.
Urusi imekataa katakata kumshutumu Rais wa Syria Bashar al-Assad katika miezi 22 ya mgogoro wa kisiasa ambao umesababisha vifo vya zaidi ya watu 60,000.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Urusi ilisema: "Kama habari hizi ni za kweli, basi itakuwa ni jambo la kuweko kwa mashambulizi yasiyo na sababu dhidi ya nchi huru, hata kama washambuliaji watakuwa na sababu zao za kufanya hivyo."
Uhusiano kati ya Urusi na Israel umeimarika katika miaka ya hivi karibuni huku ushirikiano wa kibiashara na kiuchumi ukikua, asema mwandishi wa BBC aliyeko Moscow, Stephen Rosenberg.
Moscow ni mshirika wa karibu wa Rais Assad. Israel na Marekani wamekataa kutoa taarifa yoyote kuhusu tukio hilo.

No comments:

Post a Comment