Monday, January 7, 2013

Lisu ataka ushirikiano kuleta maendeleo

MNADHIMU Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lisu amewaomba wanachama wa Chadema mkoani hapa kumwongezea nguvu Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa katika shughuli za maendeleo.

Lisu alisema hayo katika mkutano wa hadhara mwishoni wa wiki iliyopita katika viwanja vya Mwembetogwa na kuongeza kuwa imefika wakati Wanachadema kumwongezea nguvu Msigwa ili kufanikisha shughuli za maendeleo na katika uamuzi wa kimaslahi wa jimbo.

Alisema kumchagua Msigwa pekee bila kuongeza nguvu nyingine ikiwamo Madiwani wengi katika Baraza la madiwani, litasaidia kufanya uamuzi sahihi na usimamizi bora wa miradi ya maendeleo pamoja na uamuzi wa bajeti inayokuja katika Jimbo la Iringa mjini.

“ Nimefurahi kumpa ubunge Msigwa ili awawakilishe bungeni, kwani ni mtendaji mzuri na anawatetea lakini ukija huku jimboni madiwani ni wachache katika Baraza la Madiwani wapo 24 ambao wawili ndiyo wa kwetu sasa katika uamuzi hawa wenzetu wa CCM wanatushinda, sasa mtusaidie 2015 kuweka madiwani wengi ili tufanye mambo ya maana,” alisema Lisu.
Aidha alisema kupanga safu hiyo waanze na mwaka 2014 katika uchaguzi mdogo wa Serikali za mitaa, ili kumpunguzia kazi Msigwa ya kushughulikia masuala ya ngazi ya chini ili wampe nafasi kufuatilia mambo mbalimbali ya maendeleo ngazi ya kitaifa. “

Kwa sasa wapo wachache lakini wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kuwabana hawa wenzetu na maendeleo yanaonekana, lakini niwaombe sana pangeni safu ya chama chetu kuanzia katika uchaguzi mdogo wa serikali za mitaa mwakani kisha ongezeni madiwani mwaka 2015” alisema Lisu.

Wakati huo huo wanachama hao wa Chadema wamewaunga mkono wakazi wa Mtwara kufuatia serikali kutaka kuisafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Dar Es Salaam bila ya wenyewe kunufaika nayo.

Wanachama hao wa Chadema waliunga mkono wakazi wa Mtwara baada ya Lisu kuwauliza kama wanaunga mkono gesi hiyo kusafirishwa kutoka mkoa huo na kupelekwa Dar bila manufaa nayo .

“ Hii ni rasimali yetu Watazania wote, na si kama hatutaki serikali kuipeleka gesi hiyo Dar Es Salaam kisha kuirudisha Mtwara, lakini kwanini wanaisafirisha bila wao kunufaika nayo kisha ndiyo wairudishe tena huko, Wanachadema wenzangu lazima tuwaunge mkono wenzetu” alisema Lisu.

No comments:

Post a Comment