Monday, January 28, 2013

‘Sumu’ ya DK Slaa yaitesa CCM Moshi

Mwita alisisitiza kuwa kamwe CCM haiwezi kujibu hoja kwa kusukumwa na mikutano ya Chadema bali watafanya hivyo kunapokuwa na hoja na CCM iko katika mchakato wa kujibu mapigo.
Katika mkutano huo, Dk Slaa, Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari na Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), John Heche walimwaga sumu inayokifanya CCM kuweweseka.
Katika mkutano huo viongozi hao pamoja na Mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema wanadaiwa kutumia maneno makali kumshambulia Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama.
Viongozi hao wa Chadema waliwachongea Gama, Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi, Bernadette Kinabo na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Ibrahim Msengi kuwa wanaingilia utendaji wa Halmashauri.
Kauli za viongozi hao zilitokana na hotuba ya Meya wa Manispaa ya Moshi kuwashtaki viongozi hao wa serikali ya CCM kuwa wanazuia utekelezaji wa maamuzi ya baraza kwa masilahi ya kisiasa.
Meya huyo alisema viongozi hao wamekuwa wakitumia vibaya vikao vya ushauri mkoa (RCC) na vile vya wilaya(DCC) kuingilia uamuzi halali wa Manispaa ya Moshi inayoongozwa na Chadema.
Alitoa mfano wa viongozi hao kumwagiza Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Bernadette Kinabo kuendesha operesheni dhidi ya wafanyabiashara wadogo ili kuichonganisha Chadema na wananchi.
Kwa mujibu wa Meya huyo, Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo limekuwa katika wakati mgumu kutokana na Kinabo kukataa kutekeleza maazimio ya vikao halali ili tu kuinufaisha CCM kisiasa.
Mathalan alisema, sera ya Chadema Moshi Mjini ni kuwalipia ada wanafunzi wote wa sekondari ambao wazazi wao hawana uwezo, lakini mkurugenzi huyo amekataa kuidhinisha fedha hizo.
Meya huyo alisema mwaka 2011/2012, Halmashauri hiyo inayoongozwa na Chadema ilitenga Sh196 milioni kulipa ada hizo na mwaka 2012/2013 imetenga Sh216 milioni ambazo zote hazijaidhinishwa.
“Ukimuuliza anasema sera ya elimu bure siyo sera ya Serikali.Tunaomba hoja hiyo uipeleke bungeni tujue ni wakati gani vyama vinaweza kutekeleza sera zake kwa halmashauri inazoziongoza,”alisema.
Meya huyo alisema vitendo vinavyofanywa na viongozi hao wawili ni dhahiri vina lengo la kuidhoofisha Chadema kisiasa katika Jimbo la Moshi na pia kuwagombanisha na wananchi.

No comments:

Post a Comment