Saturday, November 3, 2012

Wapanda treni Dar wamtoa kijasho Mwakyembe

ABIRIA wanaotumia usafiri wa treni Dar, juzi walimtoa kijasho Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, alipokwenda kuwasimamia abiria hao wapande kwa foleni kwenye treni inayotoka Stesheni kwenda Ubungo Maziwa.Dk Mwakyembe aliwasili eneo hilo kati ya saa tisa alasiri na saa kumi na moja jioni kushuhudia usafiri huo unavyoendelea, ambapo alikutana na kadhia mbalimbali kwenye huduma hiyo mpya jijini.

Alitumia kipaza sauti kutoa maagizo kwa abiria kusimama kwenye foleni, lakini jitihada zake zilichukua muda kueleweka kwani kadri alivyokuwa akitangaza ndivyo abiria hao walivyomzonga.

“Nasema simameni kwenye foleni, kama mtu hatasimama kwenye foleni hatapanda” alisema Dk Mwakyembe mara kwa mara lakini abiria badala ya kufanya kile alichowaagiza walikuwa wakimsonga wengine kwa kutaka kumwona, wengine wakitaka kusikia anachosema.

Pengine ujio wa Waziri huyo mwenye dhamana ya usafiri ulikuwa kivutio kituoni hapo kwani alipotoa maagizo kwenye behewa moja na kuhamia behewa jingine watu walikuwa wakimfuata hali iliyosababisha usumbufu.

“Waziri sisi tumekuja mapema hapa na tulifuata utaratibu lakini kuna watu wengine wanaharibu foleni” alisema abiria mmoja, lakini hakusikika kutokana na  kelele nyingi.

Huku wakimwonyesha tiketi kuhalalisha uwepo wao kwenye foleni, Dk Mwakyembe ambaye alikuwa amesimama kwenye mlango wa kuingilia alizidi kusisitiza abiria kujipanga kwenye foleni lakini ni wachache waliomuelewa.

Baadaye kidogo alipozungumza na Maofisa wa Kampuni ya Reli(TRL) Dk Mwakyembe aliwaambia; “Tukishindwa kujiwekea misingi sasa hivi huko mbele utakuwa ugonjwa na maradhi yasiyotibika.”

“Nimetoka bungeni kwa sababu hii nije nione kinachoendelea” alisema Waziri Mwakyembe ambaye jana aliacha kikao kinachoendela mjini Dodoma kuja Dar es Salaam kwa sababu hiyo.

“ Bora wasafiri abiria 20 wenye nidhamu kuliko kupeleka abiria 300 hovyo hovyo” alisema Dk Mwakyembe ambaye alifuatana na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Mhandisi Omar Chambo.

Katika hatua nyingine MAMLAKA ya Reli  ya Tanzania na Zambia (Tazara), imeelemewa na wingi wa abiria wanaotumia usafiri huo jijini Dar es Salaam kutokana  na mwitikio mkubwa wa wananchi katika  kutumia huduma hiyo.
Hayo yameelezwa  na Ofisa Usalama wa Mamlaka hiyo, Hanya Mbawala,  alipokuwa akizungumza  na Mwananchi ofisini kwake  jana .

“Abiria wanaotumia treni ni wengi tofauti na mategemeo yetu, hii inatupa changamoto ya kuongeza idadi ya mabehewa ili kuweza kukidhi mahitaji”alisema Mbawala.

Mbawala alieleza kuwa Tazara ina mpango wa kuongeza idadi ya mabehewa saba ifikapo Machi mwakani ili kupunguza msongamano wa abiria.

“Tunatengeneza mabehewa mengine saba ambayo mpaka  Machi mwakani  yatakuwa yamekamilika, tutakuwa tukiongeza behewa moja kila linapo kamilika” alisema.

Aliongeza kuwa wanatarajia kuimarisha ulinzi ili kudhibiti abiria wasio waaminifu katika kulipa nauli baada ya kutumia usafiri huo sambamba na kurahisisha upatikanaji wa tiketi  kwa kila abiria.

Tangu kuanza kwa usafiri wa treni jijini Dar es Salaam wadau wa usafiri huo wameeleza kuwa upatikanaji wa tiketi imekuwa ni changamoto jambo ambalo linaweza likapunguza mapato kwa mamlaka husika.

Akilizungumzia suala hilo Mbawala alisema kuwa tiketi zinazo tumika zinazalishwa na kampuni ya Selcom ila wanatarajia kuwa na kikao nao kulizungumzia jambo hilo.

Utoaji wa huduma ya treni jijini hapa imeonekana kuingilia ratiba ya treni za abiria na mizigo za mamlaka hiyo hivyo kulazimu urekebishaji wa ratiba za treni hizo.

 Mamlaka hiyo inatarajia kubadilisha ratiba ya treni ya kasi (express) ambayo ilikuwa inaondoka kila siku ya Jumanne saa 9.50 alasiri na kuwa itaondoka saa 7.50 mchana siku hiyo hiyo na kwamba hakutakuwa na mabadiliko kwa treni ya kawaida.

No comments:

Post a Comment