Saturday, November 3, 2012

Wabunge kutoa maoni ya Katiba leo

WABUNGE wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo watatoa maoni yao juu ya Katiba Mpya mjini Dodoma, ikiwa ni mara ya kwanza tangu Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuanza zoezi la ukusanyaji wa maoni ya wananchi, Mei mwaka huu.
Tangu kuanza kwa zoezi hilo baadhi ya wabunge wameshatoa maoni yao baada ya Tume hiyo inayokusanya maoni nchi nzima kufika katika majimbo yao, wabunge hao ni pamoja na Tundu Lissu (Singida Mashariki) na  Shukuru Kawambwa (Bagamoyo).
Zoezi la kukusanya maoni ya wabunge hao litaongozwa na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Mstaafu Joseph Warioba Makamu wake Jaji Mkuu mstaafu Augustino Ramadhani, zoezi hilo litaanza asubuhi.
Akizungumza na wananchi wa Kata ya Iglansoni wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Jaji Ramadhani ambaye kwa sasa anaambatana na kundi la tume hiyo lililopo mkoani Singida, alisema leo itakuwa fursa kwa wabunge kutoa maoni yao.
“Nitakuwa Singida mpaka ijumaa (jana), kwa sababu Jumamosi (leo) Tume itakuwa mjini Dodoma kwa ajili ya kupata maoni ya wabunge juu ya Katiba” alisema Ramadhani.
Tume hiyo kwa nyakati tofauti imekuwa ikikutana na makundi mbalimbali kwa ajili ya kupata maoni yao kuhusu Katiba Mpya.
Makundi hayo ni pamoja na viongozi wa dini, vyombo vya ulinzi na usalama, makundi maalum na sasa ni zamu ya wabunge.
Katika hatua nyingine Jaji Ramadhani aliwatoa wasiwasi wananchi kwamba sio lazima waijue Katiba ya sasa, ndio waweze  kutoa maoni juu ya Katiba Mpya.
“Sio kweli kuwa mpaka uijue Katiba ya sasa ndio uweze kuchangia maoni ya Katiba Mpya, matatizo yanayowakabili wananchi yanahusiana moja kwa moja na Katiba na ndio hayo mnayotakiwa kuyasema” alisema Ramadhani.

No comments:

Post a Comment