MHARIRI wa Gazeti la Business Times, Mnaku Mbani amejeruhiwa kwa risasi
mdomoni na watu wanaosadikiwa kuwa majambazi akiwa njiani kwenda
nyumbani kwake Mbagala, Dar es Salaam.
Mnaku alipigwa risasi juu ya mdomo, upande wa kulia iliyotokea kwenye shavu la kushoto na kupoteza meno matatu ya juu.
Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Temeke, David Misime alisema jana kwamba tukio hilo
lilitokea saa 1:20 usiku katika eneo la Mtoni Madafu.
Alisema Mnaku
akiwa na watu wengine wanne walikuwa wanasafiri kwenye gari aina ya
Toyota Noah wakitokea mjini kuelekea Mbagala, kabla ya watu wanaodhaniwa
kuwa ni majambazi kulisimamisha na kuanza kulishambulia kwa risasi
wakidhani kuwa lilikuwa limebeba fedha.
“Walikuwa wakipiga risasi
wakiwalazimisha watoe fedha, walidhani hili gari lilikuwa likisafirisha
fedha kwa hiyo walikuwa na matumaini ya kupata maburungutu ya fedha,
walipokosa walianza kutawanyika,” alisema Kamanda Misime.
Alisema
miongoni mwa abiria hao wanne, watatu walijeruhiwa kwa risasi na wawili
kati ya hao, walipata matibabu katika Hospitali ya Temeke na kuruhusiwa
kurejea makwao, lakini Mnaku alihamishiwa katika Hospitali ya Taifa ya
Muhimbili kwa matibabu zaidi.
“Hatutajua hawa majambazi walikuwa
wangapi, lakini tunajua walikuwa zaidi ya watatu, tunachokifanya sasa
hivi ni kuwatafuta na kwa namna yoyote ile... Lazima tutawashika,”
alisema.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, uongozi wa
Kampuni ya Business Times umesema hali ya Mnaku inaendelea vizuri licha
ya kutoweza kuzungumza kutokana na maumivu aliyonayo.
“Hali ya Mnaku
inaendelea kuimarika na anaendelea kupata uchunguzi wa madaktari katika
Hospitali ya Taifa Muhimbili. Uongozi wa Makampuni ya Business Times
Limited unaendelea kufuatilia hali yake kwa karibu ili kuhakikisha
anapata huduma na uangalizi unaostahili,” imesema taarifa hiyo
iliyosainiwa na Mhariri Mtendaji wa Majira, Imma Mbuguni.
Wakili apigwa risasi Mwanza
Huko
Mwanza, Wakili wa kujitegemea wa Kampuni ya Juristic Law Chamber, Elias
Hezron amelazwa katika Chumba cha Wagonjwa wanaohitaji Uangalizi
Maalumu (ICU), katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando baada ya
kushambuliwa kwa risasi tumboni na kuporwa kompyuta ndogo (laptop).
Tukio
hilo limetokea siku chache tangu kuuawa kwa risasi kwa aliyekuwa
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow kwa risasi.
Kaimu
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Lili Matola amethibitisha kutokea kwa
tukio hilo na kusema jeshi lake linafuatilia tukio hilo na baada ya
kukamilisha uchunguzi wake, litatoa taarifa kwa vyombo vya habari.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana, wakili mwingine wa kampuni hiyo, George
Hezron ambaye ni kaka yake wa wakili huyo, alisema tukio hilo lilitokea
saa nane usiku wa kuamkia jana nyumbani kwa wakili huyo huko Nyegezi,
Wilaya ya Nyamagana.
Alisema kabla ya uvamizi huo, umeme ulikatika na
kisha wavamizi hao wanaosadikiwa kuwa walikuwa wawili walifanikiwa
kuvunja milango ya nyumba anayoishi na kumvamia. Kabla ya kumpiga
risasi, walimtaka atoe laptop yake ya ofisi ambayo amekuwa akiitumia
kutunzia nyaraka za uwakili pamoja na simu zake za mkononi.
“Wakili
aligoma kutekeleza maagizo yao na mmoja wa wavamizi hao alimpiga kwa
nondo kichwani, ndipo alipoanza kupambana. Wakati amefanikiwa
kumdhibiti mmoja, mwingine alimpiga risasi ya tumboni na wote kutoweka
na laptop hiyo pamoja na simu zake mbili na nyingine za mkewe,” alisema
Wakili George.
Alisema kwa sasa hali ya wakili huyo inaimarika licha
ya kuwa ICU akiwakariri madaktari waliomweleza kuwa risasi hiyo
haikuathiri tumbo lake kwa kiasi kikubwa na kwamba upo uwezekano wa
kupona mapema.
Kumekuwa na mfululizo wa matukio ya mauaji ya watu
katika Jiji la Mwanza tangu mwezi uliopita. Kabla ya tukio hilo la usiku
wa kuamkia jana, Oktoba 13, mwaka huu saa nane usiku, watu
wasiojulikana walimuua Kamanda Barlow katika mazingira ambayo bado
hayajafahamika chanzo chake. Tayari watu watano wameshafikishwa
mahakamani wakikabiliwa na kosa hilo.
Oktoba 9, mwaka huu Ofisa
Uhamiaji katika Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Mwanza, Albert Buchafwe
alinusurika kuuawa kwa risasi baada ya kushambuliwa na polisi saa nne
usiku eneo la Nyakato, katika kile kilichodaiwa kuwa jeshi hilo lilikuwa
likishambulia majambazi.
No comments:
Post a Comment