WANAFUNZI wa Elimu ya Juu ambao ni wanachama wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chaso) katika Tawi la Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (Teku),
mkoani Mbeya, wamelalamikia viongozi wa chama hicho kwa kutotembelea
tawi hilo tangu lilipozinduliwa.
Imeelezwa kuwa tawi hilo
lilizinduliwa na Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe Mei mwaka jana, akiwa amefuatana na
viongozi wengine wa chama hicho.
Wanafunzi hao walitoa malalamiko yao
juzi wakati wa mahafali ya pili ya wanachama wa Chaso, Tawi la Teku,
yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kiwira, jijini Mbeya na kuhudhuriwa na
viongozi mbalimbali wa chama hicho.
Akisoma risala ya wanafunzi hao,
Joseph Mlundi alisema tangu tawi hilo lilipozinduliwa mwaka jana, hakuna
kiongozi hata mmoja katika ngazi ya mkoa na wilaya, aliyewahi
kulitembelea na kuzungumza na wanachama.
“Tangu kufunguliwa kwa
Tawi la Chaso kwenye chuo chetu hatujawahi kumwona kiongozi yeyote si wa
ngazi ya wilaya wala mkoa, aliyewahi kuja kututembelea na kuzungumza na
wanachama kwa nia ya kujenga chama,” alisema Mlundi.
Alisema licha
ya wanafunzi hao kushiriki katika harakati mbalimbali za nje na ndani ya
chuo hicho, inasikitisha kuona hakuna anayeonekana kuwajali hata kwa
kuwatembelea.
Mlundi alisema pamoja na mafanikio waliyoyapata, Chaso
Tawi la Teku bado linakabiliwa na matatizo kadhaa likiwemo la ukosefu wa
fedha za kulipia pango la ofisi.
Alikiomba chama hicho ngazi ya
taifa, kutoa ruzuku hadi ngazi ya matawi ili kuwaepusha katika hatari ya
kutimuliwa kwenye jengo la ofisi.
Akizungumzia tatizo la
kutotembelewa na viongozi hao, Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema
wa Mkoa wa Mbeya, Joseph Kasambala aliwawarushia vijembe viongozi wa
wilaya na mkoani kuwa baadhi yao wanaogopa kuzungumza na wasomi.
Alisema
hali hiyo ndiyo inayosababisha wanafunzi hao kutotembelewa na hivyo
kudumaza mwamko wa mabadiliko ya kisiasa ndani ya vyuo hivyo.
No comments:
Post a Comment