UTAPELI wa aina yake, umeibuka mkoani Kilimanjaro ambapo kundi la matapeli hula njama na wanawake kuandaa mitego ya fumanizi na kujipatia mamilioni ya shilingi.
Uchunguzi wa kina wa Mwananchi Jumapili umebaini
kuwa kundi hilo limekuwa likiwalenga wanaume walio katika ndoa na wenye
uwezo wa kifedha, ambao baada ya kunaswa katika fumanizi hizo hupigwa
picha zinazogeuzwa mradi.
Utapeli huo unawalenga wafanyabiashara, watu wenye nyadhifa kwenye taasisi na hata viongozi wa dini.
Kundi hilo lenye mtandao mpana nchini, linaonekana katika siku za karibuni kujikita katika mkoa wa Kilimanjaro.
Uchunguzi huo unaonyesha kuwa katika kipindi cha
wiki mbili, watu wanne wamejikuta wakinaswa katika mtego huo na kutoa
kitita cha kati ya Sh3 milioni na Sh10 milioni, gharama hizo zikiwa nje
ya zile za kukomboa picha.
Kundi hilo hufanya kazi kwa kuwatumia wasichana
wadogo na wakubwa, ambao wanaajiriwa maalumu kwa kazi hiyo ambayo
haitofautiani na ya uchangudoa.
Mbali na waume za watu, wengine ambao wamenaswa
kwenye mtego huo ni baadhi ya mapadri wa Kanisa Katoliki, ambao
hulazimika ‘kumalizana’ nao wakihofia kuchafuliwa kwa kashfa iwapo jambo
hilo litaanikwa kwa umma.
Katika tukio la hivi karibuni, mfanyabiashara
mmoja wa mjini Moshi alinaswa katika fumanizi hilo na mwanamke mmoja
aliyedaiwa ni mkazi wa eneo la KDC Barabara Kuu ya Moshi-Himo na kulipa
Sh3 milioni.
“Kwa hofu ya taarifa kumfikia mkewe, jamaa yangu
aliamua kutoa fedha walizotaka, na unajua unapofumaniwa akili zinapotea
kwa muda na unakuwa huna ujanja,” kilidokeza chanzo chetu.
Hata hivyo, chanzo hicho kilidai kuwa baada ya
kupita wiki moja, mfanyabiashara huyo alipigiwa simu na mtu
aliyejitambulisha kuwa ni mwandishi wa gazeti moja la udaku akimtaarifu
kuwa ana picha za mfanyabiashara huyo alizopigwa kwenye
fumanizi.
“Baada ya hapo tuliifuatilia namba yake na
tumegundua anaitwa (jina tunalo), lakini kule kwenye lile gazeti
hawamfahamu kabisa wala hiyo namba hawaijui,” alidai ndugu wa
mfanyabiashara huyo.
Alidai kuwa, baada ya kumfuatilia mwanamke
anayedaiwa kufumaniwa na ndugu yao, waligundua pia kwamba, tukio hilo
ulikuwa ni mchezo mchafu.
No comments:
Post a Comment