Monday, November 5, 2012

Maandamano ya uhuru wa Biafra Nigeria

Hawa ni baadhi ya watu wanaotaka kujitawala kwa jimbo la Biafra
Takriban watu miamoja wamekamatwa Kusini Mashariki mwa Nigeria baada ya maandamano ya kuunga mkono uhuru wa jimbo lililojitenga la Biafra.
Wanachama wa vuguvugu la Biafran Zionist Movement, waliipandisha bendera ya Biafra na kisha kuandamana katika barabara kuu za mji wa Enugu.
Mmoja wa viongozi wa vuguvugu hilo, aliambia BBC kuwa watu 500 walikamatwa na wangali wanazuiliwa lakini msemaji wa polisi alisema kuwa idadi hiyo ilikuwa watu 101.
Zaidi ya watu milioni moja walifariki wakati wa vita vya Biafra kati ya mwaka 1967 na 1970.
Wengi wa waliofariki walikufa kutokana na njaa.
Vugu vugu la BZM mwanzo lilifanya mkutano siku ya Jumapili kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa kiongiozi wa Biafra Chukwuemeka Ojukwu, aliyefariki mwezi Machi.
Msemaji wa polisi wa neo la Enugu Ebere Amarizu, aliambia BBC kwamba wale waliokamatwa walikuwa wamezuiliwa ingawa alikataa kusema mashtaka wanayokabiliwa nayo.
Mwandishi wa BBC mjini Lagos Will Ross anasema kuwa baada ya miaka 45 ya bendera ya Biafra kupandishwa,
hatua iliyosababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe, idadi ndogo ya watu wangali wanataka kujitenga kwa jimbo hilo, licha ya tisho la kukabiliwa na kosa la jinai.
Mwandishi wa BBC anasema kuwa vita hivyo tena vimeanza kuangaziwa kwani mwandishi mashuhuri nchini humo
Chinua Achebe amechapisha kumbukumbu zake kuhusu vita hivyo.
chanzo-bbc.com

No comments:

Post a Comment