Monday, November 5, 2012

Askari wa Rwanda wamuua mwanajeshi wa DRC



Waasi wa M23 ambao Rwanda inadaiwa kuwaunga mkono
Rwanda imetuhumu wanajeshi kutoka Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa kufanya uchokozi baada ya kundi moja kuvuka mpaka.
Hali iliyosababisha makabiliano katika eneo tete la mpakani kati ya nchi hizo mbili. .
Mmoja wa wanajeshi wa Congo alipigwa risasi wakati mmoja wa Rwanda alijeruhiwa katika ufyatulianaji wa risasi. Tarrifa hii ni kwa mujibu wa msemaji wa jeshi.
Msemaji wa jeshi la DRC alidokeza kuwa makabiliano yalikuja baada ya wanajeshi wa DRC kuvuka mpaka kununua vileo.
Rwanda imekuwa ikikana kuhusika na vita vinavyoendelea Mashariki mwa DRC lakini wafadhili kadhaa wamesitisha msaada kwa Rwanda baada ya Umoja wa Mataifa kutoa madai kuwa wanawapa silaha waasi na kufadhili kundi la M23.
Takriban watu 500,000, wametoroka makwao Mashariki mwa DRC tangu mwezi Aprili,wakati kundi la M23 lilipoanza mapigano.
Mwandishi wa BBC Jean-Claude Mwambutsa nchini Rwanda anasema kuwa hii ndio mara ya kwanza kutokea makabiliano kati ya wanajeshi wa Rwanda na DRC tangu mwaka 2001.
Anasema kuwa huku jamii ya kimataifa ikiwa imezipiga darubini nchi hizi mbili, sio rahisi hatua kama hii kusababisha vita.
Msemaji wa jeshi la Rwanda, Brigedia Generali Joseph Nzabamwita, alisema wanajeshi kutoka DRC walikuwa wanaingia DRC kufanya uchunguzi.
"Hiki ni kitendo cha uchokozi. Wanataka kingiza Rwanda katika shida zao za ndani lakini Rwanda imekuwa ikisema haiko tayari kuchochea hali hiyo," alisema Brigedia Nzabamwita.
Makabiliano hayo yaliripotiwa kutokea karibu na eneo la Kibumba, kilomita kumi na tatu Kaskazini mwa mji wa Goma.

No comments:

Post a Comment