Wednesday, November 7, 2012

M-pesa kunufaisha zaidi Watanzania

Katika kuendeleza azma yake ya kuwawezesha wananchi kubadili maisha kupitia teknolojia ya simu za mkononi, Kampuni ya Vodacom Tanzania, sasa inawawezesha wateja wake kutumia huduma ya M-pesa kwa faida zaidi katika kila muamala wa utumaji wa pesa.

Kupitia uwezeshaji huo, mteja wa Vodacom anayetuma pesa kwa njia ya M-pesa, atapokea muda wa hewani bure ukiwa na  thamani sawa na gharama alizotozwa wakati akituma pesa hizo, kwenda sehemu yoyote nchini.

Huduma hiyo itatolewa mara baada ya mteja kumaliza kutuma pesa hizo.

Akizungumzia mpango huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Rene Meza, alisema hiyo ni moja ya njia za  kuwashukuru wateja zaidi milioni 4.5 wanaoendelea kuiamini huduma ya M-pesa na kuitumia kila siku katika shughuli zao.


“Mteja haitaji kujisajili ili kunufaika na kampeni hii na wala hatotumia muda kupokea muda wa hewani wa bure, Vodacom itampatia shukrani yake ya muda wa hewani kwa kutumia M-pesa mara tu atakapomaliza kutuma fedha hizo kwenda kwa mteja wa Vodacom katika sehemu yoyote hapa nchini,” alisema Meza.

Alisema chini ya mpango huo, wateja wa Vodacom wanapata zaidi cha kujivunia katika huduma yao ya M-pesa huku wakiwa na wigo mpana zaidi wa kufurahia mawasiliano kupitia mtandao wa Vodacom kwa kuwa na salio la ziada la kufanya hivyo.

“Ni fursa nyengine kwa wateja wetu kufurahia kila watumapo pesa kwa M-pesa huku wakipata cha ziada kufurahia kuwa wateja wa Vodacom kwa kuongea zaidi miongoni mwao,”alisisitiza.

Tangu ilipoanzishwa Aprili mwaka  2008 huduma ya M-pesa imebakia kuwa huduma bora, salama, ya uhakika na yenye kuaminika kwa Watanzania.

No comments:

Post a Comment