WAKAZI wa Kijiji cha Msijute, Halmashauri ya Wilaya Mtwara, mkoani hapa
wametaka katika Katiba ijayo, Rais aongezewe madaraka ili kumpa nguvu ya
kufanya uamuzi.
Wakitoa maoni yao mbele ya Tume ya kukusanya maoni
ya Katiba, wakazi hao bila kufafanua aina ya madaraka anayopaswa
kuongezewa Rais, walisema hawaoni umuhimu wa kupunguza madaraka ya
kiongozi huyo wa juu wa nchi.
Saidi Nawanda (62) na Selemani
Likoko (68) kwa nyakati tofauti walisema mamlaka aliyonayo Rais kwa sasa
hayatoshi hivyo ni muhimu aongezewe.
“Rais aongezewe madaraka, ili akisema jambo basi litekelezwe” alisema Nawanda bila ya kufafanua madaraka anayopaswa kuongezewa.
Maoni kama hayo pia yalitolewa na Likoko, ambaye alihoji iweje Rais apunguziwe madaraka badala ya kuongezewa.“Rais aongezewe madaraka, na kamwe asipunguziwe” alisema Likoko.
Katika
mkutano huo ulioendeshwa na mwenyekiti wa timu iliyopo hapa, Sengondo
Mvungi, ulitanguliwa na maelezo ya umuhimu wa kutoa maoni ya Katiba
yaliyotolewa na Mjumbe wa Tume hiyo, Kibibi Hassan ambaye aliwaambia ni
wakati mwafaka kwao kutengeneza Katiba waitakayo.
“Tumieni fursa
hii kutoa maoni yenu, jisikieni huru, utakachosema ndicho
kitakachonukuliwa, baada ya hapa tutarudi kwenu tukiwa na rasimu ya
Katiba, safari hiyo tutaiwasilisha kwenu kupitia mabaraza ya wilaya”
alisema Hassan.
Aliongeza kuwa “Tutaipeleka kwenye Bunge maalumu
la Katiba na baada ya hapo italetwa kwenu kwa ajili ya kupigia kura ya
ndiyo na hapana, msiwe na wasiwasi, hii ni Katiba yenu.”
MKAZI wa Kata ya Kintinku, Wilaya ya Manyoni, Hadija Ismail (58)
amependekeza Katiba Mpya iwe na kifungu kinachosema misafara yote ya
viongozi hususan Rais iwe na magari yasiyozidi 10 ili kupunguza
gharama za uendeshaji.
Hadija alisema kuwa fedha zinazotumika
kugharimia magari zaidi ya 30 yanayokuwa katika msafara mmoja wa Rais,
zinaweza kujenga madarasa na kuwalipa fedha ya ziada walimu wanaoishi
vijijini.
Akizungumza wakati akitoa maoni juu ya Katiba Mpya
juzi, Hadija alisema Katiba Mpya inatakiwa kueleza wazi suala hilo,
kwa kuwa fedha za walipa kodi ndiyo zinazotumika kuendeshea magari hayo.
“Rais
msafara wake unatakiwa kuwa na magari 10 tu, msafara wa Waziri Mkuu na
Makamu wa Rais unatakiwa kuwa na magari matano matano,” alisema Hadija.
Alisema
kuwa ni ajabu kwa viongozi wa Serikali kutumia magari mengi katika
shughuli zao za kila siku wakati kuna baadhi ya vijiji, wananchi
wanatumia jembe la mkono katika shughuli za kilimo.
“Mfano
msafara mmoja unakuwa na magari 30, ukipiga hesabu ya gharama ya mafuta
kwa magari 20, labda kutoka Dodoma mpaka Singida, zinatosha kabisa
kununulia trekta la kilimo” alisema Hadija.
Pia Hadija alisema kuwa
viongozi wote wanaochaguliwa na wananchi wanatakiwa kukaa madarakani kwa
vipindi viwili tu na siyo kama ilivyo sasa ambapo wapo wabunge wenye
miaka zaidi ya 30 bungeni.
“Diwani na mbunge nao wanatakiwa kuwa na vipindi viwili tu vya kugombea kama ilivyo kwa Rais” alisema.
No comments:
Post a Comment