Thursday, November 8, 2012

JK akumbana na mabango akizindua bomba la gesi

RAIS Jakaya Kikwete amejikuta akipokewa na mabango wakati akizindua mradi mkubwa wa bomba la gesi asilia linalotoka Mtwara hadi eneo la Kinyerezi jijini  Dar es Salaam.

Mradi huo unatarajiwa kumaliza kabisa tatizo la umeme wa mgawo ifikapo mwaka 2015 kwa kuzalisha megawati 3,000 ambazo ni zaidi ya mahitaji ya umeme kwa sasa.

Wanaume wawili waliokuwa na mabango kwenye kundi la watu zaidi ya 20, waliyanyanyua juu mabango yanayomtaka Rais Kikwete aingilie kati malipo ya fidia za viwanja na mali zitakazoathirika kwenye moja ya mradi wa gesi eneo hilo baada ya kuzungushwa kwa muda mrefu.

Tukio hilo lilitokea wakati Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik akitoa hotuba ya kuwakaribisha wageni na kuelezea umuhimu wa mradi huo kwa wakazi wa Dar es Salaam.

Watu hao walinyoosha juu mabango hayo kuelekea jukwaa kuu, alikokuwa amekaa Rais Kikwete jambo lililosababisha maofisa usalama kuwaamuru washushe chini, lakini kundi hilo lilianza kuzomea hivyo kusababisha usikivu hafifu kwenye  mkutano huo uliohudhuriwa na mamia ya wananchi.

Kuona hivyo, Mkuu wa Mkoa alisitisha hotuba yake na kutoa ufafanuzi juu ya madai hayo akisema taarifa za madai yao tayari wanazo na zinashughulikiwa kuanzia leo.

Sadick aliwasisitizia kuwa kitendo walichokifanya wakazi hao siyo sahihi kwa sababu madai yao hayahusu mradi ambao unazinduliwa na Rais Kikwete bali kampuni binafsi ya Kilwa Energy ambayo ipo kwenye mchakato wa kuwekeza katika mradi wa kuzalisha umeme.

“Madai yenu tunayajua na tayari tumeanza kuyashughulikia, lakini mnapaswa kufahamu kuwa madai yenu hayahusu mradi huu ambao Mheshimiwa Rais anauzindua leo,” alisema Sadick na kuongeza:

“Madai yenu yanahusu mradi wa kampuni binafsi ya Kilwa Energy ambao bado haujasainiwa. Tumekwisha kukubaliana kesho (leo) tutakutana na viongozi wenu kujadili.”

Moja ya bango lilisomeka: “Mtukufu Rais tunaomba utusaidie malipo ya fidia ya viwanja vyetu maana tumezunguswa muda mrefu.”

No comments:

Post a Comment