RAIS Jakaya Kikwete amejikuta akipokewa na mabango wakati akizindua
mradi mkubwa wa bomba la gesi asilia linalotoka Mtwara hadi eneo la
Kinyerezi jijini Dar es Salaam.
Mradi huo unatarajiwa kumaliza
kabisa tatizo la umeme wa mgawo ifikapo mwaka 2015 kwa kuzalisha
megawati 3,000 ambazo ni zaidi ya mahitaji ya umeme kwa sasa.
Wanaume
wawili waliokuwa na mabango kwenye kundi la watu zaidi ya 20,
waliyanyanyua juu mabango yanayomtaka Rais Kikwete aingilie kati malipo
ya fidia za viwanja na mali zitakazoathirika kwenye moja ya mradi wa
gesi eneo hilo baada ya kuzungushwa kwa muda mrefu.
Tukio hilo
lilitokea wakati Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik akitoa
hotuba ya kuwakaribisha wageni na kuelezea umuhimu wa mradi huo kwa
wakazi wa Dar es Salaam.
Watu hao walinyoosha juu mabango hayo
kuelekea jukwaa kuu, alikokuwa amekaa Rais Kikwete jambo lililosababisha
maofisa usalama kuwaamuru washushe chini, lakini kundi hilo lilianza
kuzomea hivyo kusababisha usikivu hafifu kwenye mkutano huo
uliohudhuriwa na mamia ya wananchi.
Kuona hivyo, Mkuu wa Mkoa
alisitisha hotuba yake na kutoa ufafanuzi juu ya madai hayo akisema
taarifa za madai yao tayari wanazo na zinashughulikiwa kuanzia leo.
Sadick
aliwasisitizia kuwa kitendo walichokifanya wakazi hao siyo sahihi kwa
sababu madai yao hayahusu mradi ambao unazinduliwa na Rais Kikwete bali
kampuni binafsi ya Kilwa Energy ambayo ipo kwenye mchakato wa kuwekeza
katika mradi wa kuzalisha umeme.
“Madai yenu tunayajua na tayari
tumeanza kuyashughulikia, lakini mnapaswa kufahamu kuwa madai yenu
hayahusu mradi huu ambao Mheshimiwa Rais anauzindua leo,” alisema Sadick
na kuongeza:
“Madai yenu yanahusu mradi wa kampuni binafsi ya
Kilwa Energy ambao bado haujasainiwa. Tumekwisha kukubaliana kesho (leo)
tutakutana na viongozi wenu kujadili.”
Moja ya bango lilisomeka: “Mtukufu Rais tunaomba utusaidie malipo ya fidia ya viwanja vyetu maana tumezunguswa muda mrefu.”
No comments:
Post a Comment