Mhadhiri mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT),
Profesa Mwesiga Baregu, amesema kuwa Tanzania inapaswa kujifunza kutoka
kwenye uchaguzi uliofanyika nchini Marekani juzi, ili kuepuka matumizi
makubwa ya fedha ndani ya vyama.
Akizungumza na Tanzania Daima jana kwa njia ya simu, Profesa Baregu,
alisema kuwa uchaguzi wa Marekani umemalizika huku kukiwa na matumizi
makubwa ya fedha kwa vyama hivyo viwili, hivyo Tanzania inapaswa
kujiepusha na mfumo huo.
Baregu ambaye pia ni mjumbe wa kamati ya kukusanya maoni ya Katiba
Mpya, alifafanua kuwa hapa nchini kumekuwa na matatizo ya matumizi ya
fedha hatua inayowafanya baadhi ya Watanzania kuogopa kuwania uongozi.
Alisema kuwa, iwapo tatizo hilo halitadhibitiwa ndani ya vyama, kuna
uwezekano mkubwa kwa watakaowania uongozi kuwa ni watu walio na uwezo wa
kifedha.
Msomi huyo ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, aliongeza
kuwa iwapo kutakuwa na udhibiti wa matumizi ya fedha katika chaguzi
mbalimbali, kundi kubwa litaweza kugombea uongozi na hivyo demokrasia
kuzidi kukua.
“Kama kutakuwepo na matumizi makubwa ya fedha hata watakaogombea
itaonyesha kuwa hawachaguliwi, bali wananunua uongozi,” alisema.
Naye, Mchungaji William Mwamalanga alisema kuwa, jambo kubwa la
kujifunza kwa Marekani ni kwa wanasiasa wa Tanzania kuwa tayari kukubali
matokeo pale wanaposhindwa ili kujiepusha na matumizi ya rushwa katika
chaguzi.
Alisema kuwa taifa la Marekani limepiga hatua kutokana na kujiepusha
na matumizi ya rushwa kwani wagombea wote hujinadi kwa sera zao kuliko
ilivyo kwa hapa nchini.
Mwamalanga alisema hatua ya kuendelea kuikumbatia rushwa, watu
kushindwa kujitokeza katika kuchagua viongozi, ndiyo sababu ya idadi ya
wapigakura kuzidi kushuka mwaka hadi mwaka.
“Tumeona wenzetu walivyoweka utaifa mbele kuliko vyama, watu wanaenda
kusikiliza kampeni na kuhoji sera na wala hakuna vibendera maana
wanautanguliza utaifa mbele,” alisema.
Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi nchini (Tucta), Nicholaus
Mgaya, aliupongeza uchaguzi wa Marekani uliomwezesha Rais Obama kurejea
madarakani, na kuitaka Tanzania kuiga mfano huo.
Akizungumza na Tanzania Daima kuhusu uchaguzi huo, alisema demokrasia
imechukua mkondo wake kwani kushinda ni mambo ya kawaida, kusionekane
chama fulani ndicho chenye kushinda wakati wote hata kama hakifai.
Alitoa rai kwa serikali kutokuwa na mawazo kwamba wakati wa uchaguzi chama kingine kikiingia madarakani kitaharibu nchi.
Mgaya alisema uchaguzi wa Marekani uwe funzo kwa wapigakura nchini
kufuata nyayo zao kwa kuwa na uwezo wa kuamua kumchagua kiongozi
wanayemtaka kulingana na uwezo wake.
Mwananchi mwingine, Abdullah Saiwaad, alisifu demokrasia iliyotumika
wakati wa uchaguzi huo hasa kuheshimiana kati ya wagombea.
Saiwaad ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Readit Books, alimsifu
hasimu wa Obama, Romney kutokana na kukubali matokeo alipoona anaelekea
kushindwa.
Pia alisifu hotuba ya Obama kukubali kushirikiana na watu wa Republican kutafuta umoja.
“Uchaguzi huo ni mfano wa kuigwa kwa sababu tunatofautiana katika
kuchagua, lakini lazima anayeshindwa atoe ushirikiano kwa aliyeshinda
ili kujenga Tanzania yenye maendeleo,” alisema.
No comments:
Post a Comment