Saturday, November 3, 2012

Spika Makinda njia panda • Ripoti ya Jairo, Kamati ya Ngwilizi zamweka pabaya

MWENENDO wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anne Makinda, kukalia taarifa za utekelezaji wa maazimio mbalimbali ya Bunge, unamweka katika wakati mgumu, Tanzania Daima Jumapili limebaini.
Hadi sasa taarifa za utekelezaji wa maazimio makubwa matano zimekaliwa, kubwa ikiwemo ripoti inayohusu utekelezaji wa maagizo ya Bunge kuhusu tuhuma zinazomkabili aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo na taarifa ya Kamati ndogo ya Bunge ya uchunguzi dhidi ya wabunge wa Kamati ya Nishati na Madini, iliyoongozwa na Mbunge wa Mlalo, Brigedia mstaafu Hassan Ngwilizi (CCM).
Kamati ya Ngwilizi tayari imeshakabidhi taarifa yake kwa Spika Makinda, lakini hadi sasa inafanywa kuwa siri.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa, taarifa ya ripoti ya Ngwilizi haitaletwa bungeni licha ya presha kutoka kwa wabunge, hasa wa Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa.
Sababu inayotajwa ya kutowasilisha taarifa hiyo bungeni, ni kutokana na madai kuwa ripoti hiyo imechakachuliwa na mafisadi.
Wiki iliyopita, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) alitoa hoja ya jambo linalohusiana na Haki za Bunge kwa mujibu wa kanuni ya 55 (3) (f) na 59 (e) ya kutaka Bunge lipewe haki yake kwa haraka ya kupewa taarifa na Spika juu ya hatma ya Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini kwa kuzingatia kuwa tayari amekabidhiwa ripoti ya Kamati ya Ngwilizi.
Mnyika alieleza kwamba, matatizo ya mafuta na gesi asili yanayoendelea sasa ni matokeo ya udhaifu wa serikali katika kutekeleza maazimio na mapendekezo ya Bunge, huku kukiwa hakuna Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ili kuweza kuisimamia serikali kwenye sekta ya nishati, na hivyo kuathiri uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.
Iwapo hoja hiyo iliyoungwa mkono ingejadiliwa, Spika angelazimika kueleza hatma ya Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, na kwa kufanya hivyo angelazimika pia kueleza ni kwanini ripoti ya kamati juu ya tuhuma za wabunge haijawasilishwa bungeni na ni lini itawasilishwa.
Mbali ya taarifa ya Kamati ya Ngwilizi, uchunguzi umebaini kuwa, katika kipindi cha kati ya mwaka 2008 hadi sasa, Bunge limeshindwa kupata taarifa ya maazimio makubwa matano ambayo hayajatekelezwa kwa ukamilifu, na Spika hajasimamia kuhakikisha Bunge ama kwa kupitia kamati zake, linapatiwa taarifa.
Taarifa ya serikali inayosubiriwa kwa hamu bungeni ni ile inayohusu utekelezaji wa maagizo ya Bunge kuhusu tuhuma za Jairo.
Ikumbukwe kwamba, Novemba 2011, Bunge lilipitisha maazimio ya hatua za kuchukuliwa baada ya Kamati Teule ya Bunge iliyoundwa kuchunguza uhalali wa utaratibu wa Wizara ya Nishati na Madini kuchangisha fedha kwa ajili ya kupitisha bajeti bungeni ya mwaka 2011.
Kumbukumbu za Bunge zinaonyesha kuwa, Spika Makinda aliikataa taarifa ya ripoti hiyo kwa vile majibu ya serikali hayakumridhisha.
Hata hivyo, hadi sasa hajaitaka serikali kuwasilisha taarifa hiyo kwenye mikutano iliyofuata kuanzia ule wa bajeti wa mwezi Juni mpaka Agosti 2012 na hata huu wa sasa unaoendelea, ratiba inaoonyesha kwamba taarifa ya Jairo imewekwa kabatini.
Tuhuma dhidi ya Jairo ziliibuka wakati Wizara ya Nishati na Madini ilipokuwa inawasilisha bajeti kwa mwaka wa fedha 2011/12 ambapo Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo (CCM) alidai kuwa alichangisha sh bilioni moja kutoka kwenye taasisi mbalimbali zilizo chini ya wizara yake kwa ajili ya kusaidia kupitisha bajeti hiyo.
Baada ya madai hayo, serikali ilichunguza suala hilo kupitia Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utoah, na hatimaye uamuzi kutangazwa na aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo, kuwa Jairo hakuwa na makosa na akamwamuru arejee kazini.
Bunge halikuridhika na hali hiyo na kuunda Kamati Teule ya Bunge ambayo ilimtia Jairo hatiani na kupendekeza maazimio mbalimbali ya serikali kutekelezwa ambayo mpaka sasa serikali haijaeleza bungeni utekelezaji wake.
Akizungumzia suala hilo jana, Mnyika ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, alisema kuwa inaonyesha kwamba serikali bado haioni uharaka na ulazima wa kuchukua hatua, hivyo ni muhimu Spika atumie madaraka na mamlaka yake kuiagiza iwasilishe ripoti hiyo bungeni.
“Wakati Bunge lilipokaa kama kamati tarehe 28 Julai 2012 kupitisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, nilitaka ufafanuzi kutoka kwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kuhusu utekelezaji wa maazimio hayo ambayo mpaka sasa hakuna taarifa ya utekelezaji iliyowasilishwa bungeni tangu yapitishwe Novemba mwaka 2011.
“Waziri akajibu tu kwamba hawezi kufanyia kazi taarifa za magazetini, bila kujali kwamba nilichouliza hakihusu taarifa za magazetini bali maazimio ya Bunge baada ya kazi iliyofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, na ikarudiwa tena na Kamati Teule ya Bunge ambayo ilihoji wahusika na kupata pia vielelezo. Spika anapaswa kuchukua hatua,” amefafanua Mnyika.
chanzo-Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment