Sunday, November 11, 2012

Mnyika: Spika amefunika kombe • Akata rufaa, adai adhabu zilizotolewa ndogo

MBUNGE wa Ubungo na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika, ameamua kulivalia njuga suala la tuhuma za wabunge na wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini kujihusisha na vitendo vya rushwa, akisema kuwa uamuzi wa Spika Anne Makinda umeacha makando kando mengi, ikiwemo ukiukwaji wa katiba ya nchi, hivyo anajipanga kuukatia rufaa.
Alisema kuwa uamuzi wa Spika Makinda uliotangazwa juzi bungeni, umefanyika kwa namna ya ‘funika kombe’, hivyo rufaa yake inalenga kutaka taarifa kamili ya Kamati Ndogo ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge iwasilishwe kwa ukamilifu wake kwenye kamati husika ya kudumu ya Bunge na kujadiliwa bungeni ili ‘mbivu na mbovu’ katika usimamizi na uendeshaji wa sekta ya nishati zijulikane, kisha uchunguzi wa kina ukihusisha vyombo vingine nje ya Bunge, ufanyike.
Alifafanua kwa kurejea hotuba yake aliyosoma bungeni kwa niaba ya kambi rasmi ya upinzani bungeni wakati wa Bunge la bajeti lililopita, akisema kuwa alitoa angalizo tangu awali kuwa ili ukweli ujulikane ilipaswa kuundwa Kamati Teule ya Bunge kuchunguza masuala yote ya ukiukwaji wa sheria, matumizi mabaya ya madaraka na tuhuma za ufisadi katika utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme na ununuzi wa mafuta kwa ajili ya mitambo ya umeme.
Alisema ni muhimu kufanyika kwa uchunguzi wa namna hiyo, ukihusisha pia Mkaguzi Mkuu kufanya ukaguzi wa kiuchunguzi kwa malipo yaliyofanywa na makampuni ya BP (Sasa Puma Energy), Oryx na Camel Oil ili kubaini iwapo kuna vigogo zaidi wa serikali waliojinufaisha kwa kisingizio cha dharura ya umeme, kwa kuzingatia masharti ya ibara ya 27(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, siku moja tu baada ya Spika Makinda kutoa uamuzi wake bungeni juu ya tuhuma za wabunge kujihusisha na rushwa, Mnyika alisema kuwa atakata rufaa kwa kuwa kiwango cha ‘adhabu’ kilichotolewa na Spika hakilingani na ‘makosa’ ambayo yameelezwa kuwa na uzito wenye kuathiri “kwa kiasi kikubwa hadhi ya Bunge kama taasisi na heshima ya wabunge waliohusishwa”.
Akitolea mfano, Mnyika alisema kuwa ikiwa ni kweli Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi kuwa amefanya makosa ya kuvunja haki za Bunge kwa kuzusha tuhuma za uongo ili kujihami dhidi ya wabunge waliokuwa wanahoji utendaji wake, basi adhabu aliyopewa hailingani na ukubwa wa makosa anayodaiwa kufanya.
“Kwa kosa hilo ikiwa maelezo ya Spika kuhusu matokeo ya uchunguzi wa kamati ni sahihi, anapaswa kufunguliwa mashtaka kwa mujibu wa Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki za Bunge na kupewa adhabu ya zaidi ya onyo ikiwemo hata faini au kifungo au walau kutakiwa kuwajibika.
“Kadhalika Spika ameeleza kuwa mbinu aliyotumia (Maswi) ni pamoja na kutaka kuwalipa fedha wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini shilingi milioni mbili kwa kila mjumbe, madai haya ni ya jaribio la kufanya ufisadi wa fedha na matumizi mabaya ya madaraka kama ilivyokuwa kwenye kashfa ya Katibu Mkuu aliyemtangulia, David Jairo, hivyo Spika alipaswa kupendekeza kwa mamlaka ya uteuzi wake kuchukua hatua za kinidhamu na kisheria.
“Baada ya uamuzi wa Spika kuhusu tuhuma kwamba baadhi wa wabunge na wajumbe wa kamati ya Nishati na Madini walijihusisha na vitendo vya rushwa katika kutekeleza kazi zao za kibunge, nimeulizwa na baadhi ya wanahabari na wananchi kwa simu na kwenye mitandao ya kijamii sababu za kusimama bungeni tarehe 9 Novemba 2012 mara baada ya Spika kutoa uamuzi huo na kutaka kuomba muongozo.
“Nakusudia kukata rufaa kwa sababu uamuzi wake una maudhui kadhaa yasiyozingatia katiba ya nchi, sheria mbalimbali za nchi, kanuni za kudumu za Bunge, maamuzi ya awali ya maspika wa Bunge pamoja na mila na desturi za mabunge mengine yenye utaratibu wa kibunge unaofanana na utaratibu wa bunge letu,” alisema Mnyika na kuongeza;
“Kwa kuzingatia kuwa rufaa huchukua muda kusikilizwa, nilitaka niombe muongozo wake kwa kuwa katika uamuzi wake hakueleza hatma ya Kamati ya Nishati na Madini, hivyo Spika anapaswa kuueleza umma iwapo kamati hiyo inarejeshwa au inaundwa kamati nyingine au kuelekeza kamati nyingine ya kudumu ya Bunge inayopaswa kuisimamia serikali wakati huu ambapo nchi inakabiliwa na matatizo mengi kwenye sekta za nishati na madini yenye athari kwa maisha ya wananchi.”
Aliongeza kusema kuwa, kwa kuwa katika uamuzi wake Spika Makinda alieleza kwamba Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wake Maswi wametoa maelezo yasiyokuwa kweli kwa nyakati mbalimbali, uwepo wa Kamati ya Bunge kwa ajili ya kuisimamia wizara hiyo kwa niaba ya Bunge ni suala linalohitaji uamuzi wa haraka kutokana na hali ya nchi juu ya sekta ya nishati kuwa tete bila usimamizi wa kibunge.
Aidha, katika taarifa yake hiyo, Mnyika ameonekana kushangazwa na kitendo cha Spika Makinda kutoa onyo kali kwa Katibu Mkuu na wabunge kadhaa, lakini hakutoa onyo kwa Waziri wa Nishati na Madini wala hakueleza chochote iwapo alipokea ushauri kutoka kwa Kamati Ndogo ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusu ukiukwaji wa kanuni uliofanywa bungeni wakati wa kadhia nzima.
Akikumbushia hadidu rejea moja tu iliyopewa Kamati Ndogo iliyofanya uchunguzi ya “Kuchunguza na kumshauri Spika iwapo tuhuma kwa baadhi ya wabunge na wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini kujihusisha na vitendo vya rushwa ni za kweli au hapana”, hivyo, kwa mujibu wake, baada ya uchunguzi na kuwasilisha ripoti yake Spika alipaswa kuanzisha mchakato wa adhabu, kama kulibainika kuwepo kwa makosa ya ukiukwaji wa kanuni.
Alisema kuwa uamuzi wa Spika ‘kufunika kombe’ hauna tofauti na maamuzi yaliyotangulia ambayo yamesababisha mpaka sasa serikali haijawasilisha bungeni ripoti ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge juu ya sakata la aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Jairo, kufuatia uchunguzi uliofanywa na Kamati Teule ya Bunge.
Aliongeza kuwa, leo ataeleza masuala ya ziada atakayoyakatia rufaa na kauli yake kuhusu maelezo na uamuzi wa Spika juu ya Waziri na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini.

No comments:

Post a Comment