Saturday, November 3, 2012

JK aikataa ramani ya Jiji Arusha

RAIS Jakaya Kikwete ameikataa ramani ya awali ya Jiji la Arusha iliyowasilishwa ofisini kwake, baada ya kugundua kuwa haiko kiuhalisia baada ya kujumuisha maeneo ya vijiji vyenye shughuli ya kilimo na ufugaji visivyoruhusiwa ndani ya Jiji.

Akihutubia mkutano wake wa kwanza wa hadhara mjini Arusha tangu mwaka 2010, mara baada ya kuzindua Jiji la Arusha juzi, Rais Kikwete aliuagiza uongozi wa Jiji na serikali mkoani Arusha kuandaa ramani mpya itakayozingatia na kukidhi mahitaji na uhalisia kwa kuondoa maeneo ya vijiji.

Aliuambia umati wa wananchi waliohudhuria mkutano uliofanyika uwanja Sheikh Amri Abeid kuwa ramani ya awali aliyoikataa inataja Manispaa tatu zitakazounda Jiji la Arusha kuwa ni Arumeru Mashariki,Arumeru Magharibi na Arusha Mjini.

ìKwa tafsiri hiyo ina maana maeneo ya vijiji kama Ngarenanyuki,Oldonyo Sambu na sehemu zingine ambazo shughuli kuu ya wananchi ni kilimo na ufugaji ambayo kisheria hayaruhusiwi ndani ya Jiji yatakuwa sehemu ya Jiji la Arusha,î alisema Rais Kikwete

Wakazi wengi wa wilaya ya Arumeru inayoundwa na Halmashauri za Meru (Arumeru Mashariki) na Arusha DC (Arumeru Magharibi) ni wafugaji kutoka makabila ya Kimaasai, Kiarusha na Kimeru ambao njia yao kuu ya uchumi ni ufugaji wa kuchunga na kilimo.

Iwapo, Rais angekubaliana na ramani iliyowasilishwa kwake, shughuli
zote za ufugaji na kilimo zingepigwa marufuku na hivyo kuathiri maisha ya wananchi wengi wa wilaya ya Arumeru, ambao wangelazimika kutafuta njia nyingine ya kumudu maisha yao, jambo ambalo lingeibua mgogoro wa kimaslahi kati yao na serikali.

Kabla ya kupanda hadhi kuwa Jiji, eneo la Halmashauri ya Manispaa ya Arusha ilikuwa ni Kilomita za Mraba 93. Eneo hilo limeongezeka hadi kufikia Kilomita za Mraba 208 baada ya baadhi ya sehemu na Kata za wilaya ya Arumeru kumegwa na kuhamishiwa wilaya ya Arusha.

Katika hatua nyingine, Waziri wa Ujenzi, Dk Jahn Magufuli, ameuagiza uongozi wa Jiji la Arusha kuhakikisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami unaoendelea Jijini humo unazingatia mahitaji na kukua kwa mji kwa zaidi ya miaka 50 ijayo.

ìBarabara za Jiji zinatakiwa kuwa za njia tatu, nne na hata nane kwa kutilia maanani mahitaji na kukua kwa miji. Tusijenge barabara za kubanabana kama vile Jiji letu halitakua,î alisema Dk Magufuli.

Barabara kadhaa zenye urefu wa zaidi ya kilomita 14 za Jiji la Arusha ziko kwenye ujenzi kwa kiwango cha lami ikiwa ni mpango wa maboresho ya miji nchini unadhaminiwa na mikopo kutoka Benki ya Dunia (WB), taasisi na wadau wa maendeleo.

Wakati Dk Magufuli akitaka ujenzi wa barabara za Jiji kuzingatia mahitaji ya miaka 50 ijayo, Jiji la Arusha linakabiliwa na changamoto ya kutoweza kupanua barabara zake za katikati ya Jiji hata kufikia njia mbili kutokana na barabara zote kuu kuzingirwa na maghorofa
ambayo gharama ya kuzibomoa zinaweza kutoka kuanzisha mji mwngine mpya.

No comments:

Post a Comment