Thursday, November 8, 2012

Tanzania One sasa kuachia wazawa asilimia 50

BARAZA la Madiwani wa Halmashauri Wilaya ya Simanjiro, mkoani Manyara, limeridhia asilimia 50 ya hisa za Kampuni ya TanzaniteOne zigawanywe kabla ya kampuni hiyo kupewa upya leseni ya uchimbaji madini.
Akisoma azimio hilo kwenye Baraza la hilo juzi, Makamu mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Jackson Sipitek alisema wadau wengine wanatakiwa kupata hisa ya asilimia 50 kama sheria mpya ya madini ya mwaka 2010 inavyoelekeza.
Sipitek alisema Kampuni ya TanzaniteOne itabakiwa na asilimia 50 ya hisa,  zilizosalia zitagawanywa kwa halmashauri ya wilaya hiyo na nyingine zitauzwa kwa wananchi kupitia soko la hisa.
Alisema hisa nyingine zilizobakia zitauzwa kwa wafanyakazi wa kampuni hiyo na nyingine kwenye Wizara ya Nishati na Madini kupitia Shirika la Madini la Taifa (Stamico).
Alisema Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango ya Halmashauri ya Wilaya na baraza hilo waliwateua viongozi wanne kukutana na Wizara ya Nishati na Madini, TanzaniteOne na wadau wengine kujadili jambo hilo.
Aliwataja viongozi hao kuwa, ni Mbunge wa jimbo hilo, Christopher Ole Sendeka, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo, Peter Tendee, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri, Muhammed Nkya na Mweka hazina wa wilaya, Peter Mollel.
Hali hiyo inahitimisha sintofahamu ya muda mrefu baina ya wachimbaji wadogo na serikali, baada ya wachimbaji hao kudai kutokana na leseni ya kampuni hiyo kumaliza muda wake Agosti mwaka huu, watapatiwa eneo hilo.
Wachimbaji hao wadogo walidai kuwa, walitarajia serikali itasikia kilio chao cha muda mrefu cha kuwapatia eneo hilo, kwani madini ya vito hasa Tanzanite hayapaswi kuchimbwa na wageni.
Walisema Rais Jakaya Kikwete mwaka 2010 alipokuwa anaomba kura mjini Orkesumet, wilayani Simanjiro aliwaahidi baada ya leseni ya kampuni hiyo kumaliza muda wake atawapa eneo hilo, ahadi ambayo hajaitekeleza.
Hata hivyo, sheria mpya ya madini ya mwaka 2010 ambayo ilipitishwa na Bunge baada ya mapendekezo ya Tume ya Jaji Mark Bomani ya mwaka 2008, inaeleza madini hayo yakichimbwa na wageni wamiliki asilimia 50 ya hisa na wazawa 50.

No comments:

Post a Comment