Monday, November 5, 2012

Ripoti ya Ngwilizi kuwasilishwa • Katibu wa Bunge asema ni wakati wowote,wanakamati waliochunguzwa tumbo joto.

KATIBU wa Bunge Dk. Thomas Kashililah, amesema kuwa taarifa kuhusu ripoti ya kamati ndogo iliyoundwa kuchunguza tuhuma za wabunge kujihusisha na vitendo vya rushwa, itawasilishwa bungeni siku yoyote kuanzia leo katika mkutano unaoendelea sasa.
Dk. Kashililah aliyasema hayo katika mahojiano maalumu na gazeti hili, akitakiwa kufafanua kuhusiana na ripoti hiyo na kile kinachoaminika kuwa ni msimamo wa Spika Anne Makinda, kutotaka ripoti hiyo isisomwe bungeni.
“Kwa mujibu wa Sheria ya 296 inayohusu Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge hili jambo linahusu haki, ni lazima taarifa yake itawasilishwa,” alisisitiza Dk. Kashililah.
Hata hivyo, licha ya kulihakikishia gazeti hili kuwa ripoti hiyo itawasilishwa bungeni lakini alikataa kutaja ni siku husika na kusisitiza kuwa tayari Spika amekwishaifanyia kazi.
Dk. Kashililah alisema Spika hajaing’ang’ania ripoti hiyo kama ambavyo wengi wamekuwa wakiamini na kwamba uamuzi wowote utakaofanywa kuhusu ripoti hiyo utakuwa ni wa wazi.
Alisema baada ya Spika kuifanyia kazi ripoti hiyo, ataamua kama yeye aiwasilishe au airudishe kwenye kamati hiyo iliyokuwa ikiongozwa na Brigedia Hassan Ngwilizi, itoe taarifa.
Kuhusu taarifa ya ripoti hiyo kutokuwamo kwenye ratiba za shughuli za Bunge, Dk. Kashililah alisema hilo halimzuii Spika kupanga utaratibu wake wa kuipeleka bungeni.
“Spika anapotaka kuliingiza jambo kwenye shughuli za Bunge hahitaji kuliweka katika ratiba, atakapoamua itaingizwa kwenye Order Paper (ratiba inayoonyesha shughuli za Bunge kwa siku)…mamlaka anayo, anaweza kurekebisha,” alisema.
Kwa mujibu wa ratiba ya mkutano wa tisa wa Bunge, leo baada ya kipindi cha maswali na majibu, utawasilishwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria mbalimbali ya mwaka 2012.
Kesho baada ya kipindi cha maswali, kutakuwa na tathmini ya matumizi ya Kanuni za Kudumu za Bunge siku ambayo pia huenda suala la taarifa ya ripoti hiyo ya Ngwilizi ikaingizwa kwenye ratiba.
Alhamisi ratiba inaonyesha kuwa kutakuwa na maswali kwa Waziri Mkuu na baada ya hapo, yatafuata maswali ya kawaida kisha hoja binafsi za wabunge na Ijumaa baada ya maswali kutakuwa na hoja binafsi za wabunge kabla ya kuahirisha Bunge.
Tangu kamati ya Ngwilizi imalize uchunguzi wake na kukabidhi ripoti kwa Spika, kumekuwepo na taarifa kadhaa zikidai kuwa Makinda anakataa ripoti hiyo isijadiliwe kwa maelezo kuwa anahitaji muda kuifanyia kazi.
Makinda alitoa uamuzi wakati wa kikao cha wabunge wote kilichokuwa kikijadili ratiba ya shughuli za Bunge hili la tisa.
Bila kutoa ufafanuzi wa kina, Spika Makinda alisema yeye ndiye anajua lini na wakati gani wa kuileta hoja hiyo bungeni na kamwe hawezi kuileta kwa shinikizo la wabunge.
Hata hivyo, hatua hiyo iliibua maswali kutoka kwa baadhi ya wabunge waliotaka kujua sababu za kutoileta ripoti hiyo ijadiliwe bungeni, lakini Spika hakutaka kutoa ufafanuzi na badala yake alisisitiza kwamba haitajadiliwa katika mkutano huo wa Bunge.
Makinda anaelezwa kuwa asingeweza kuileta ripoti hiyo bungeni kwani uchunguzi umebaini hakuna mbunge aliyejihusisha na rushwa wakati tayari alishavunja Kamati ya Nishati na Madini kwa tuhuma hizo.
Wajumbe wengine waliomo kwenye kamati ya Ngwilizi ambaye pia ni mbunge wa Mlalo ni Saidi Arfi (Mpanda Kati), John Chiligati (Manyoni Mashariki), Goesbert Blandes (Karagwe) na Riziki Omary Juma (Viti Maalumu).
chanzo-Tanzania daima

No comments:

Post a Comment