Tuesday, November 13, 2012

Ndesamburo azungumzia afya yake

MBUNGE wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo (Chadema), amethibitisha kuwa anaumwa na anapatiwa matibabu nchini Uingereza.


Hata hivyo, amesema hadi jana alikuwa anaendelea vizuri na anasubiri uamuzi wa daktari wake kumruhusu atoke hospitalini. Ndesamburo alitoa kauli hiyo alipokuwa anazungumza na gazeti hili juzi usiku.

“Ni kweli naumwa, lakini sijazidiwa hata kidogo si hata wewe (mwandishi) si unanisikia ninaongea na wewe vizuri kabisa ningekuwa nimezidiwa tusingeongea hivi,” alisema Ndesamburo.

Mbunge huyo amewatoa hofu wananchi wa Jimbo lake kuwa afya yake ni imara baada ya kupatiwa matibabu na mara madaktari wake watakapomruhusu atarejea nchini.

Hata hivyo, Ndesamburo hakuweka wazi ugonjwa unaomsumbua, lakini akisisitiza kuwa suala la kuumwa kwa binadamu ni la kawaida na kwamba hali yake kwa sasa ni nzuri.

Wakati Ndesamburo akithibitisha kuugua, Katibu wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro, Basil Lema jana alilijia juu gazeti hili akihoji sababu za kuandika habari ya kuumwa kwa Ndesamburo.

Hata baada ya mwandishi kumweleza katibu huyo Ndesamburo ni kiongozi wa umma hivyo watu wake wanapaswa kufahamu alipo, bado aliendelea kuhoji kwa nini iliandikwa akisema habari hiyo ilikuwa na agenda ya kisiasa nyuma yake.

Ndesamburo hajaonekana katika jukwaa la siasa kwa karibu mwezi mmoja sasa, hali iliyotafsiriwa ndiyo iliyochochea baadhi ya watu kuvumisha kuwa hali yake ni mbaya.

Mbunge huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro, hakuhudhuria vikao vya Bunge lililomalizika Ijumaa kutokana na kuwapo kwake nje ya nchi.

Mkurugenzi wa Idara ya Shughuli za Bunge, John Joel aliliambia gazeti hili jana kwamba ofisi ya Bunge ina taarifa kuhusu Ndesamburo kwenda kumwona daktari wake nje ya nchi, kwa ajili ya uangalizi wa kawaida, lakini siyo kwamba alikuwa mgonjwa sana.

“Ofisi ya Bunge ina taarifa kwamba Mheshimiwa Ndesamburo alikwenda nje ya nchi kumwona daktari, maana aliwahi kutibiwa huko na alikuwa ameambiwa kwenda tena huko, kwa hiyo siyo kwamba yuko mahututi ni uangalizi wa kawaida wa afya yake,” alisema Joel.

No comments:

Post a Comment