Friday, December 27, 2013

Zitto: Siwataji walioficha mabilioni Uswisi ng’o

Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe amevunja ukimya na kusema hayuko tayari kwa sasa kuwataja Watanzania wenye mabilioni huko Uswisi na kuitaka Serikali ifanye uchunguzi.
Zitto ndiye aliyeibua hoja bungeni kuwa kuna Watanzania walioficha Sh315 bilioni katika taasisi za fedha nchini Uswisi.
 
Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe. 

Katika taarifa yake aliyoitoa jana, Zitto alisema anasita kutaja majina hayo sasa ili kuepusha kile alichosema majina hayo kutumiwa vibaya bila kujali kama Watanzania walizipata fedha hizo kihalali au la na kuzihifadhi nje ya nchi.
Alisema ameshauri mchunguzi wa kimataifa anafaa kufanya kazi hiyo.
Mbunge huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), amesema wastani wa Sh729.3 bilioni hutoroshwa kila mwaka kwenda nje ya nchi.
Alisema kauli ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Fredrick Werema kwamba yeye (Zitto) hakutoa ushirikiano wa kamati inayochunguza sakata hilo si ya kweli.
“Nataka niwahakikishie, nimekutana mara nne na kamati hii. Nimewapa mpaka jina la mchunguzi wa kimataifa atakayeweza kuwasaidia katika uchunguzi huu, leo naambiwa sitoi ushirikiano,” alisema Zitto.
Alisema mchunguzi huyo wa kimataifa ana uzoefu katika uchunguzi wa suala kama hilo na angeweza kuwatambua kwa majina na kiasi cha fedha na pia uhalali na uharamu wa fedha hizo.
Alisema ameshangazwa na hatua ya Serikali kumbeza pale alipopendekeza suala la kutafutwa mchunguzi wa kimataifa lakini siku chache baadaye ikatangaza magazetini nafasi ya kazi hiyo.
Tangazo hilo lilichapwa Desemba 17, mwaka huu siku ambayo Zitto alisema kwamba angesoma maelezo binafsi kujibu kauli ya Jaji Werema. Hata hivyo, alisema alikosa nafasi. Zitto amesema hashurutishwi na azimio la Bunge kutaja majina hayo kwa sababu yeye siyo chombo cha uchunguzi ambacho kinapaswa kuwa na mkono mrefu.
Alisema wakati akikabidhi majina ya Watanzania hao, angependa ushahidi huo uwe umefanyiwa uhakiki na vyanzo vyake vya kimataifa na vyombo vya usalama vya Serikali nchini.
“Siko tayari kutaja kwa sasa. Narudia tena kwa sasa hayo majina maana naweza kusababisha wahukumiwe na umma bila kupitia utaratibu uliowekwa na sheria zetu hapa nchini,” alisema Zitto.

No comments:

Post a Comment