Sunday, December 1, 2013

Suala la udini na ukabila ndani ya CHADEMA kuendana na mtizamo na mawazo yangu-Albert Msando

Leo ni tarehe 1/12/2013. Mwezi wa mwisho wa mwaka 2013. Ni siku ya Jumapili.

Nimeonelea vyema niongelee suala (sio hoja) la udini na ukabila ndani ya CHADEMA kuendana na mtizamo na mawazo yangu ambavyo kwa pamoja vinasababisha msimamo wangu binafsi.

Kumekuwa na malalamiko na manung'uniko mengi kwamba CHADEMA ni chama cha kidini na kikabila (baadae ilibadilika ikawa kikanda). Majibu au maelezo yametolewa kila mara lakini kama ilivyo kawaida bado maswali yapo.

Kwa nini udini na ukabila? Kuna ukweli au ni hisia? Hakuna ukweli ila ni hisia ambazo ni sahihi kuwepo (justified concerns).

Udini na ukabila ni masuala ambayo hayakubaliki sehemu yeyote ile katika jamii yetu. Ni dhambi. Pia ni kosa kumbagua au kumpendelea mtu kwa sababu ya kabila lake au dini yake ambayo kwake yeye yako sawa kabisa.

Udini:

Kwenye siasa vyama viwili vimeandamwa sana kuhusu udini. Chadema na CUF. Kwamba kimoja ni cha Wakristo kingine cha Waislamu.

Chanzo:

Kwa tafakari yangu ya juu juu hii ni kwa sababu ya sura ya uongozi wa juu wa vyama hivi. Chadema imekuwa na viongozi wengi Wakristo wakati CUF imekuwa na viongozi wengi Waislamu. Hii inajumuisha wabunge wa vyama hivi vyote viwili!! Mfano Chadema ina Wakristo wengi zaidi ya Waislamu (wengine walikuwa wachungaji na bado wanaitwa hivyo) na CUF ina Waislamu wengi zaidi ya Wakristo.

Pia vyama hivi vimejikuta vina wafuasi katika maeneo ambayo ni waumini wa dini mojawapo jambo ambalo linafanya hayo mawazo yapate nguvu zaidi. Kwa mfano CUF maeneo ya Tanga na Zanzibar na Chadema maeneo ya Kilimanjaro nk.

Jambo jingine ni viongozi wa dini hizi mbili pia wamekuwa wakionekana kujitanabaisha na viongozi wa vyama hivi kwenye matukio na shughuli mbalimbali.

Kwa mfano, utakuta kanisa linamualika kiongozi mkristo wa Chadema kwenye Harambee au kiongozi wa Chadema anahudhuria msiba wa kiongozi wa dini mkristo lakini hautamsikia kiongozi huyo akihudhuria Harambee ya msikiti au mazishi ya kiongozi wa dini ya Kiislamu. And vice versa is also true.

Mawazo na hisia zinajengeka hapo...ni vigumu kuepuka hisia na mawazo kujengeka kati hali kama hiyo.

Hiyo haitokani na ukweli kwamba kiongozi huyo mkristo au muislamu ni mdini bali inatokana na uwezo mdogo wa kiongozi husika kuona madhara ya kushindwa kutambua hatari ya hisia hasi kwa matendo yake.

Chadema (tuache CUF) kwa kiasi kikubwa tumeshindwa kuvuka mstari na kuwafikia waumini wa Kiislamu aidha kwa kupitia viongozi wetu Wakristo au viongozi wetu Waislamu ili kuwathibitishia kwamba chama chetu hakina agenda ya dini.

Ni tabia ya mwanadamu kumsikiliza na kumfuata yule ambaye wana jambo linalofanana kwa wepesi zaidi kuliko yule ambaye ni mtu wa mbali au hawafanani. Hivyo mara nyingi binadamu atamsikiliza au kumfuata yule ambaye anajipambanua kwamba atamtetea maslahi yake. Sio kwa sababu ni mdini ila kwa sababu anajisikia salama zaidi yeye binafsi na pia anaona anamsaidia 'mwenzake'.

Hatuwezi kuepuka uwepo wa hizo hisia kama hatutachukua hatua stahiki. Tukibaki kujidanganya kwamba ni propaganda tatizo halitaondoka badala yake haitakuwa hisia tena ila ukweli mchungu na itatuathiri umoja wetu kama chama na taifa kwa ujumla.

Malalamiko ya udini yapo na yanatokana na sababu ambazo baadhi nimezitaja. Ila sababu KUBWA ni utashi wa viongozi wakati wa maamuzi. Mara nyingi huwa hawaangalii tafsiri atakayotoa mwanachama au Mwananchi kuhusu maamuzi fulani kwenye masuala ambayo yatagusa dini au imani yake.

Mfano, ni kiongozi gani amelisimamia waziwazi suala la mahakama ya kadhi kwenye Katiba mpya? Ni nani amesema anakubali au anakataa mahakama ya kadhi?

Hatuna viongozi ambao wanajipambanua kwa MISIMAMO yao kuhusu mambo ambayo ni ya msingi kwa Mwananchi. Tuna viongozi ambao tunapenda kujificha kwenye kichaka cha 'kauli ya chama' 'ilani ya uchaguzi' 'msemaji wa chama' 'sera ya chama' nk.

Ni nadra sana utamsikia kiongozi akisema 'Mimi Albert Msando naunga mkono uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi. Mimi ni mkristo lakini naamini kwamba Waislamu wanastahili kuwa na mahakama yao'. Wengi wetu hatuthubutu.

Chadema haina udini hata kidogo. Ila inashindwa kuondoa hisia hizo kwa kuchukua hatua badala ya matamko na kukanusha. Ni lazima tukae chini na viongozi wa Waislamu na madhehebu mengine kuwaeleza kwamba hatuna agenda ya siri dhidi ya Uislamu au Waislamu na pia hatuna agenda ya siri kwa faida ya Wakristo au Ukristo. Tuwaeleze malengo na nia yetu kuleta maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi.

Ukabila:

Hili sababu ni kama za suala la kidini ila lenyewe ni matokeo ya uzembe zaidi. Tunaliacha liendelee bila sababu zozote za msingi.

Chadema haiko Kilimanjaro au kanda ya kaskazini peke yake. Ni kweli ina wabunge wengi kutoka upande huu lakini pia kama chama kipo kila kona ya Tanzania bara.

Tunaweza kujitetea kuhusu nafasi za uchaguzi lakini ni uzembe kuteua aidha wabunge au viongozi kutoka kanda ya kaskazini. Siamini kwamba wenye uwezo na mapenzi mema na Chadema wako kaskazini peke yake. Tunaweza kuteua viongozi kutoka maeneo mengine kwa idadi kubwa na kusema wazi kwamba mpango huo ni kuweka usawa katika uwakilishi. Sio KOSA!!!

Viongozi wetu wana changamoto ya kuweka mpango kazi kuthibitishia wanachama na watanzania kwa ujumla kwamba sisi Chadema sio wadini wala wakabila(wakanda).

Pia sioni sababu ya Mzee Mtei kuendelea kutoa matamko kuhusu maamuzi au mwenendo wa Chadema kwa umma. Anaweza kutoa ushauri au hata maelekezo kwa viongozi bila kutangazia umma.

Mwananchi wa kawaida kwa msaada wa adui yetu anaruhusiwa kuwa na hisia kwamba chama ni cha Mbowe na Mtei! Kwa sababu tu Mbowe amemuoa mtoto wa Mtei. Jambo ambalo ni ukweli kwamba Mbowe ameoa kwa Mtei. Lakini kuoa sio sababu ya kusema eti chama ni cha familia. Sisi wote hatuwezi kuwa wajinga kiasi cha kukubali hilo! Ni upuuzi kusema tunaweza kuruhusu.

Mimi binafsi Mbowe ni msimamizi wa ndoa yangu. Lakini sio sababu ya mimi kuwa mwanachadema au Diwani wa Chadema. Na siwezi kuacha kumkosoa kama atakosea kwa sababu tu ni msimamizi wangu. Mambo yetu ya kifamilia hayana nafasi kwenye mambo ya chama. Lazima tutoke kwenye makoti yetu na tuseme waziwazi kuhusu hili jambo na tuache kufanya teuzi ambazo zinajenga sura ya ukabila au ukanda.

Msimamo wangu:

Chadema sio chama cha kidini wala kikanda. Kila mtanzania ana haki na nafasi ndani ya Chadema.

Ni jukumu la viongozi wote kuhakikisha kwamba udini na ukanda havipewi nafasi. Matendo yetu kwa yale tunayoyasimamia na uteuzi tunaofanya yaonyeshe sura hiyo. Huu ni WAJIBU wa kiongozi mwenye kuitakia mema Chadema na nchi yetu.

Tuache porojo na siasa kwa kutoa majibu mepesi pale tunaposhutumiwa. Tufanye kwa vitendo. Let us attack the problem.


AGM 2013 Dec.

No comments:

Post a Comment