Friday, December 27, 2013

Wakili Minde ashauri gharama za kufungua kesi zipunguzwe

Moshi. Wakili maarufu mkoani Kilimonjaro, Elizabeth Minde, ameliomba Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, kuangalia upya sheria ya gharama za kufungua kesi mahakamani ambazo alisema zimepanda mno na kusababisha wananchi wa kipato cha chini, kushindwa kufungua kesi pale wanapoona haki yao imepokonywa.
Minde ambaye pia ni Mkurugenzi wa shirika lisilokuwa la kiserikali la Haki za Binadamu, Usawa wa Jinsia na Msaada wa Kisheria mkoani Kilimanjaro (Kwieco), alisema kupanda kwa gharama za kufungua kesi, ni moja ya sababu za wananchi kushindwa kupata haki zao.
Alisema kwa sasa gharama za kufungua kesi kwa baadhi ya mashauri, zimepanda na kwamba kesi moja inaweza kufunguliwa kwa gharama ya kati ya Sh5,000 na Sh120,000 kiasi ambacho ni kikubwa kwa mwananchi wa kipato cha chini.
“Wananchi wengi hasa wa pembezoni wanashindwa kudai haki mahakamani kutokana na kupanda kwa gharama za kufungua kesi. Ilikuwa Sh.2000 lakini sasa zimepandishwa bila kuangalia wananchi watamudu vipi,” alisema.
Wakili huyo alisema kuna haja kwa Jaji Mkuu wa Tanzania kuangalia namna ya kuwasaidia wananchi wanaotafuta haki zao mahakamani. Akizungumzia utendaji kazi wa shirika lake, Minde alisema katika kipindi cha mwaka huu, shirika limefanikiwa kutoa huduma ya ushauri wa kisheria kwa wananchi 2,011.
Pia alisema shirika limefanikiwa kuwajengea uwezo wateja 513 katika kuandaa nyaraka za mahakama na vielelezo muhimu vinavyohitajika mahakamani na kwamba watatumia ujuzi huo katika kupigania haki zao

No comments:

Post a Comment