Thursday, September 6, 2012

CHADEMA-Waikataa Tume ya Nchimbi

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeiponda tume ya Dk Nchimbi kikieleza kuwa imeundwa ili kurudisha uhusiano kati ya Polisi na waandishi wa habari na si kutafuta chanzo cha tatizo.

Juzi, Dk Nchimbi alitangaza kamati ya kuchunguza mauaji hayo inayoongozwa na Jaji Mstaafu, Steven Ihema na wajumbe, Mwakilishi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Theophil Makunga, Mwakilishi wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Pili Mtambalike, Mtaalamu wa milipuko kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kanali Wema Wapo na Naibu Kamishna wa Polisi (DCP), Isaya Mngulu.

Mkurugenzi wa Sheria, Katiba na Haki za Binadamu wa Chadema, Tundu Lissu alisema Dar es Salaam jana kwamba: “Hii si tume ya kuchunguza mauaji, bali ina lengo la kurudisha uhusiano mzuri kati ya Jeshi la Polisi na waandishi wa habari ili kuwasahaulisha wananchi kwa sababu imeundwa na waziri ambaye naye anatakiwa kuhojiwa.” “Tunamwomba Rais Jakaya Kikwete ateue tume kama anavyoelekezwa na Sheria ya Tume za Uchunguzi ya mwaka 1992, ambayo inaruhusu kumhoji yeyote kasoro yeye Rais.”

Lissu alisema Rais Kikwete angeunda tume hiyo na Waziri Nchimbi na IGP Said Mwema wanatakiwa kujiuzulu ili kupisha uchunguzi akidai kwamba kuna uwezekano mkubwa kwamba walitoa amri ya mauaji hayo.
“Dk Nchimbi anatakiwa kumuiga Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi ambaye alijiuzulu akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani baada ya kutokea mauaji, akijiuzulu atajijengea heshima tofauti na sasa kwani wananchi wamesikitishwa na mauaji hayo,” alisema Lissu.

Mwanasheria wa Chadema, Mabere Marando alidai kwamba kuna mkakati uliowekwa na Serikali wa kukidhoofisha Chadema baada ya kuonekana kwamba ni tishio kwa CCM.

Mbali na Chadema, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), pia limesema halina imani na kamati hiyo likisema imekuwa kawaida kwa Serikali kuunda tume ambazo hazileti ripoti kwa wananchi.
“Tume zimekuwa zikiundwa bila faida yoyote, huku zikipewa muda kuchunguza yaliyotokea lakini matokeo yake huwa hakuna ripoti wanayorudisha,” alisema Kaimu Katibu Mkuu wa Tucta, Hezron Kaaya.

Kaaya alisema tume zimekuwa zikiundwa na kuigharimu Serikali fedha nyingi za walipa kodi, lakini ripoti zake zinaendelea kuwa siri.

Imeandikwa na Habiel Chidawali, Dodoma, Hamida Sharrif Morogoro, na Tumaini Msowoya, Iringa na
Lasteck Alfred na Juliana Malondo.

No comments:

Post a Comment