Tuesday, September 25, 2012

WAKATI KIKWETE AKIJINASIBU KWAMBA CCM IPO IMARA,HABARI ZA UCHUNGUZI ZINASEMA VIGOGO WENGI WAPO KATIKA HATI HATI YAKUFUTWA KATIKA ORODHA YA WAGOMBEA.

MADAI ya utabiri wa kifo cha Chama cha Mapinduzi (CCM), yamemfikia Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, ambaye amejigamba kuwa wanaotabiri kifo hicho, watakufa wao kabla chama.
Rais Kikwete alitoa majigambo hayo jana wakati akifungua kikao cha Kamati Kuu ya (CC) mjini hapa, kilichofanyika katika ukumbi wa makao chama hicho.
Alisema kuwa kikao cha Kamati ya Maadili kilichomalizika jana saa 9 alfajiri kilikuwa na majina mengi ambayo yalitakiwa kupitiwa kwa umakini zaidi ili kuweza kutenda haki kwa walioomba nafasi mbalimbali za kugombea uongozi ndani ya CCM.
Rais alifafanua kuwa licha ya kuwepo kwa majina mengi ya wagombea nafasi mbalimbali lakini kikao hicho kimeweza kufanya mabadiliko tofauti na mapendekezo yaliyotoka mikoani.
“Tumefanya kazi kubwa sana katika kupitia majina ya waliopitishwa kugombea nafasi ya Halmashauri Kuu (NEC) kutoka mikoani kwanza walikuwa wengi na wasomi pia walikuwepo wengi.
“Hata kikao cha maadili tumepitia majina ya wagombea kwa umakini na kufanya mabadiliko tofauti na mapendekezo ambayo yaliletwa kutoka mikoani, tumejaribu kujihoji ni kwa nini huyu kapewa alama hii na huyu kanyimwa alama hii,” alisema Kikwete.
Alisema kuwa Kamati ya Maadili ilikuwa ikipitia jina moja hadi jingine, na yamefanyika mabadiliko ya mapendekezo ya wagombea kutoka ngazi za mikoani.
 “Kikao cha Kamati ya Maadili kilikuwa kikubwa zaidi na chenye kuhitaji umakini mkubwa na ndiyo maana tulimaliza saa 9 alfajiri, lengo lilikuwa ni kupitia majina kwa usahihi lakini kikao hiki natarajia kitakuwa chepesi na kitaisha mapema saa 6 usiku, wajumbe msiwe na wasiwasi,” alisema Kikwete.


Kauli ya Rais Kikwete kuwa Kamati ya Maadili imeyapitia majina yote moja baada ya jingine na kufanya mabadiliko tofauti na mapendekezo yaliyotoka mikoani, inaelezwa kuanza kuwaweka matumbo moto baadhi ya vigogo.
Tanzania Daima imedokezwa kuwa kumekuwa na shinikizo kubwa ndani ya chama la kumtaka Rais Kikwete kuwatosa baadhi ya vigogo kwa kukata majina yao kutokana na tuhuma mbalimbali zinazowakabili ili wasigombee.
Majina yanayotajwa kufikishwa kwa Rais ili yapigwe panga ni pamoja na Edward Lowassa anayewania ujumbe wa NEC Wilaya ya Monduli na Andrew Chenge ambaye amepita bila kupingwa huko Bariadi.
Kwa upande wa vijana wanatajwa ni Makamu Mwenyekiti wa sasa wa UVCCM, Beno Malisa, Hussein Bashe, Anthony Mavunde, Jaml Kassim, Salum Salehe na Fred Lowassa ambao inasemekana wanatumiwa kama mawakala kumwaga fedha za kuhakikisha maslahi kambi ya kigogo mmoja inaimarika kuelekea uchaguzi mkuu 2015.

No comments:

Post a Comment